2014-04-26 16:01:58

Waziri mkuu wa Ukraine Arseniy Yatsenyuk akutana na Papa mjini Vatican


Baba Mtakatifu Francisko, Jumamosi tarehe 26 Aprili 2014 amekutana na kuzungumza na Waziri mkuu wa Ukraine Bwana Arseniy Yatsenyuk na baadaye alikuwa na mazungumzo na Kardinali Pietro Parolin aliyekuwa ameambatana na Askofu mkuu Dominique Mamberti, Katibu mkuu wa mambo ya nchi za nje na ushirikiano wa kimataifa mjini Vatican.

Mazungumzo ya viongozi hawa wawili yalijikita katika masuala ya uhusiano kati ya pande hizi mbili; hali tete inayoendelea kujitokeza nchini Ukraine, kwa matumaini kwamba, wadau wote watajitahidi kushirikiana ili kurejesha hali ya amani na utulivu mintarafu sheria za kimataifa pamoja na kudumisha uhusiano mwema kati ya watu.

Kwa namna ya pekee, viongozi hawa wawili wamegusia mchango wa Makanisa na Mashirika ya kidini nchini Ukraine na kwamba, wanachangamotishwa kutekeleza majukumu yao kikamilifu katika mchakato wa ujenzi wa amani na utulivu. Viongozi hawa wameonesha uwezekano wa Jumuiya ya Kimataifa kushiriki zaidi katika mchakato huu.







All the contents on this site are copyrighted ©.