2014-04-25 10:00:30

Changamoto kubwa ni: Umissionari na Uinjilishaji Mpya!


Askofu mkuu Josephat Lebulu wa Jimbo kuu la Arusha katika mahojiano maalum na Radio Vatican anakiri kwamba, Mwenyeheri Yohane XXIII alikuwa ni kiongozi mnyenyekevu, hodari na shupavu, aliyethubutu kuleta mabadiliko makubwa katika maisha na utume wa Kanisa kwa kuitisha maadhimisho ya Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican. RealAudioMP3

Hapa Papa Yohane XXIII akafungua malango ya Kanisa Katoliki kwa Roho Mtakatifu akapita katika maisha na utume wa Kanisa na matunda yake, wengi wanayashuhudia wakati huu.

Askofu mkuu Lebulu anasema, licha ya Papa Yohane Paulo II kumteuwa kuwa Askofu, alibahatika kuwa naye karibu wakati wa hija yake ya kichungaji nchini Tanzania. Wakati huo, Askofu mkuu Lebulu, alikuwa ni Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania. Hii ni hija ambayo imeacha chapa kubwa katika maisha na utume wa Kanisa Katoliki Tanzania. Papa Yohane Paulo II aliwapatia maneno ya faraja na matumaini makubwa, akiwataka Maaskofu kuwa imara katika imani, ili waweze kuwaimarisha ndugu zao katika Kristo. Kwa hakika amekuwa ni kiongozi mashuhuri na mfano wa kuigwa katika maisha na utume wake.

Yohane Paulo II alikuwa ni kiongozi mnyenyekevu, mwenye upendo mkubwa na aliyewajali watu wake; akampenda Kristo na Kanisa lake, kiasi cha kujitosa kimasomaso bila hata ya kujibakiza chembe! Askofu mkuu Lebulu anasema kwamba, Kristo ndiye anayewaongoza watu wake, lakini pia kwa mifano bora ya maisha na utume wa watakatifu, watu wengi wanavutwa kumfuasa Kristo vizuri zaidi.

Padre Raymond Saba, Katibu mkuu wa Baraza la Maaskofu Katoliki anasema kwamba, changamoto kubwa na endelevu ambayo imeachwa na Mwenyeheri Yohane Paulo II ni Umissionari na Uinjilishaji Mpya, unaojikita katika ushuhuda wa maisha kwa njia ya imani tendaji, kama alivyofanya Yohane Paulo II wakati wa uhai wake. Ni Kiongozi aliyetamani kuona kwamba, Kristo anawafikia watu wengi zaidi, ili kuwaonjesha upendo na uwepo endelevu wa Kristo kati ya watu wake.

Ni Kiongozi aliyethubutu kuwajengea uwezo waamini kumfungulia Kristo malangao ya maisha yao ili Kristo aweze kuwapatia dira na mwongozo wa maisha. Hii ikawa kama kauli mbiu yake katika maisha na utume wake katika mchakato wa Uinjilishaji Mpya.

Maendeleo na ustawi wa Kanisa la Tanzania ni sehemu ya mchango wa dhati kabisa uliotolewa na Mwenyeheri Yohane Paulo II aliyebahatika kuitembelea Tanzania na kuzungumza na watanzania katika Majimbo makuu ya: Dar es Salaam, Songea, Tabora, Mwanza na Jimbo Katoliki la Moshi. Maaskofu wengi ambao bado wako madarakani wakiongoza Majimbo mbali mbali nchini Tanzania, ni matunda ya Mwenyeheri Yohane Paulo II na baadhi yao ni wale ambao wameteuliwa hivi karibuni na Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI.

Ni matumaini ya Padre Raymond Saba kwamba, Papa Francisko atawateulia Maaskofu wengine wapya ili kuziba mapengo ya Maaskofu katika Majimbo matano ambayo hadi sasa yako wazi kutokana na sababu mbali mbali za kichungaji.







All the contents on this site are copyrighted ©.