2014-04-24 08:45:56

Sera zinazokumbatia utamaduni wa kifo si sahihi kwa maendeleo ya binadamu!


Askofu mkuu Francis Chullikat, Mwakilishi wa kudumu wa Vatican kwenye Umoja wa Mataifa, hivi karibuni akichangia hoja kwenye mkutano wa arobaini na saba wa Tume ya Umoja wa Mataifa inayoshughulikia watu na maendeleo anasema kwamba, kuna haja ya kusaidia familia ili kufikia maendeleo makubwa. RealAudioMP3

Kuna idadi kubwa ya watu wanaoendelea kuzeeka kwa kasi na kwa upande mwingine kuna ongezeko kidogo la watoto wanaozaliwa hususan kwenye nchi zilizoendelea zaidi duniani, hizi ni pande mbili ambazo zinapaswa kufanyiwa kazi kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya mtu mzima. Ili kuweza kuwasaidia wazee kuishi kwa amani na utulivu kuna haja ya kuwa na vijana wa kizazi kipya wanaothubutu kujenga na kutunza familia zao, ili kuchagia pia katika shughuli za uzalishaji na uchumi.

Askofu mkuu Chullikati anasema, inasikitisha kuona kwamba, kuna baadhi ya Serikali zinaona mwanamke kubeba mimba kama ugonjwa unaopaswa kupewa kinga au tiba. Hili ni jambo linalotafakarisha sana viongozi wa Seikali za Ulaya, lakini mwono wa jumla ni kwamba ongezeko la idadi ya watu linachangia pia katika mikakati ya maendeleo endelevu.

Kumbe, kuna haja ya kuwa na mwelekeo mpya katika mipango ya uzazi, badala ya kudhibiti uzazi kwa sera zinazokumbatia utamaduni wa kifo, basi, Jumuiya ya Kimataifa ijielekeze zaidi katika mikakati ya maendeleo endelevu ya binadamu; kwa kuboresha huduma ya elimu, afya, maji sanjari na kuibua sera ambazo ni rafiki kwa tunu msingi za maisha ya kifamilia. Haya ni mambo msingi ambayo yanapaswa kupewa kipaumbele cha pekee katika sera na mikakati ya maendeleo ya mwanadamu.

Askofu mkuu Chullikati anasema, sera za haki ya uzazi salama, kimsingi zinakumbatia utamaduni wa kifo kwa kuendekeza utoaji mimba, jambo ambalo linakwenda kinyume kabisa cha haki msingi za binadamu. Serikali zinapaswa kuwasaidia wanawake wajawazito kusimama kidete kulinda na kutetea zawadi ya uhai badala ya kuwasaidia katika mchakato wa utoaji mimba kwa njia ya sheria. Baba Mtakatifu Francisko anasema, si mwelekeo sahihi wa kutaka kutatua matatizo ya kijamii kwa njia ya mauaji ya watoto wasiokuwa na hatia.

Jumuiya ya Kimataifa inapaswa kuwekeza zaidi katika maboresho ya huduma za afya, elimu, chakula na lishe bora, kwa kuheshimu na kuzingatia haki msingi za binadamu pamoja na kuguswa na mahangaiko ya maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii. Sera za utoaji mimba si mkakati sahihi wa maendeleo endelevu!








All the contents on this site are copyrighted ©.