2014-04-24 10:20:44

Maaskofu Katoliki Kusini mwa Afrika waanza hija ya kitume mjini Vatican


Baraza la Maaskofu Katoliki Kusini mwa Afrika, SACBC, lililoanzishwa kunako Mwaka 1947 linaundwa na Nchi za Afrika ya Kusini, Bostwana na Swaziland. Maaskofu kutoka Kusini mwa Afrika kuanzia tarehe 24 hadi tarehe 26 Aprili 2014 wako mjini Vatican kwa ajili ya hija ya kitume inayofanyika walau kila baada ya miaka mitano.

Kanisa Katoliki Kusini mwa Afrika linaundwa na Majimbo makuu 5 yanayoyajumuisha majimbo 20. Takwimu zinaonesha kwamba, Idadi ya waamini wa Kanisa Katoliki ni sawa na asilimia kati ya 7- 8% ya idadi ya wananchi wote wa Afrika ya Kusini.

Baraza la Maaskofu Katoliki Kusini mwa Afrika kwa miaka mingi limekuwa mstari wa mbele katika mapambano dhidi ya utawala wa ubaguzi wa rangi, demokrasia ya kweli, haki na amani. Kanisa Katoliki limeendelea kuwa mdau mkubwa katika mapambano dhidi ya ugonjwa wa Ukwimi, Kusini mwa Afrika. Limejikita pia katika mapambano dhidi ya ukanimungu unaosababishwa na maendeleo ya sayansi na teknolojia katika ulimwengu wa utandawazi. Kanisa limesimama kidete kulinda na kutetea utu na heshima ya binadamu kwa kukataa katu katu utamaduni wa kifo na nyanyaso dhidi ya wanawake na watoto Kusini mwa Afrika.

Kanisa Katoliki limeendelea kujielekeza katika mchakato wa kutafuta: haki, amani na upatanisho wa kitaifa mintarafu nyaraza ya Sinodi za Afrika pamoja na kujikita katika Uinjilishaji Mpya, unaotoa kipaumbele cha kwanza kwa waamini kutolea ushuhuda wa imani yao kwa Kristo na Kanisa lake, kama chachu ya kuyatakatifuza malimwengu pamoja na kumhudumia mtu mzima katika mahitaji yake msingi. Maaskofu wanaendelea kukazia umuhimu wa kuwa na demokrasia ya kweli pamoja na kusimamia ustawi na mafao ya wengi; ukweli na uwazi, nidhamu na uwajibikaji.

Baraza la Maaskofu Katoliki Kusini mwa Afrika, Alhamisi tarehe 24 Aprili 2014 linakutana na kuzungumza na Baba Mtakatifu Francisko mjini Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.