2014-04-23 08:22:53

Kwa njia ya kazi mwanadamu anashiriki kazi ya uumbaji na ukombozi


Karol Jozef (Yozef) Wojtyla alizaliwa tarehe 18 Mei 1920 mjini Wadowice karibu na mji wa Krakovia kusini mwa nchi ya Poland, na alikuwa mtoto wa mwisho kati ya watoto watatu. Kwa bahati mbaya , hakubahatika kuwafahamu ndugu zake, kwani walifariki dunia kabla ya yeye kuzaliwa. RealAudioMP3

Akiwa na umri wa miaka tisa (9), mama yake alifariki dunia na kumuacha mtoto huyo akilelewa na baba yake, ambaye pia alifariki dunia wakati Karol akiwa na umri wa miaka 21, mnamo mwaka 1941. Mazingira ya kijamii alimokulia Karol: mnamo mwaka 1939 Vita vya Pili vya Dunia vilikuwa tayari vimekwisha anza na nchi yake ilivamiwa na Wajermani mnamo mwaka 1939, na kipindi hicho chicho nchi hiyo pia ilichukuliwa na Wakomunisti.

Katika kipindi hiki cha vita, kijana Karol alifanya kazi kama mhudumu wa hoteli ili kuweza kujiendeleza na masomo yake. Kuanzia mwaka wa 1940, kwa takriban miaka minne, Karol alisoma kwenye seminari ya kificho (kutokana na kwamba wakomunisti walifunga na kukataza maeneo ya ibada na seminari zilitekwa), na mnamo tarehe mosi Nov.1946 akapata daraja la upadre. Aliteuliwa kuwa Askofu mnamo mwaka 1958; akateuliwa kuwa Kardinali wa Jimbo kuu la Krakovia mnamo mwaka 1967; mnamo tarehe 16 Oktoba 1978 akachaguliwa kuliongoza Kanisa Katoliki kama Khalifa wa Mtakatifu Petro, hadi Mwenyezi Mungu alipomwita kwenye makao ya milele mnamo tarehe 2 Aprili 2005.

Mchango wake katika kuendeleza mafundisho jamii ya Kanisa ulijidhihirisha wazi katika mahubiri yake aliyotoa kwenye mahubiri ya misa yake ya kwanza kama papa aliposimikwa rasmi kuliongoza Kanisa Katoliki. Mchango huo unajisìdhihirisha kwenye mahubiri yake alipowaambia waumini wa Kanisa katoliki na wale wote waliokuwa wamekusanyika kwenye uwanja wa Kanisa Kuu la mtakatifu Petro mjini Vatican: Ndugu zangu, msiwe na hofu ya kumkaribisha Kristo na kukubali mamlaka yake. Na kwa uwezo wa mamlaka ya Kristo mumtumikie mwanadamu na ulimwengu mzima. Msiogope. Mfungulieni Kristo milango ya mioyo yenu, kwani ndiye pekee anayejua kile kilichopo ndani ya moyo wa mwandamu. Ni Kristo tu anayejua. Mruhusuni Kristo aongee ndani ya mioyo yenu na ndani ya moyo wa kila mwanadamu.
Kwa kupokea mamlaka yatokayo kwa Kristo, Papa Yohane Paulo II aliweza kuongea na moyo wa kila mwanadamu kwa njia ya mafundisho aliyoyatoa kama kiongozi wa Kanisa, na mchango wake katika kukabiliana na hali halisi ilivyokuwa kikanisa, kijamii na kimataifa wakati akiwa kama Khalifa wa Mtakatifu Petro. Alitoa mchango wake katika jamii kwa njia ya nyaraka mbili zilizohusu mafundisho jamii ya kanisa, ambazo ni Laborem Exercens (Kazi ya mikono ya mwanadamu), na Solicitudo Rei Socialis (Kuhusu maswala ya jamii).

Tunaweza kujiuliza kwamba, ni kwanini papa aandike waraka kuhusu kazi ya mikono ya mwanadamu, au kuhusu maswala ya jamii? Ili kuelewa nyaraka hizi vizuri, tunapaswa kufanya rejea, walau kwa kifupi tu kuhusu hali halisi ilivyokuwa kimataifa wakati papa alipochaguliwa kuliongoza Kanisa Katoliki. Tuko kwenye kipindi cha miaka ya 1980. Uchumi wa nchi tajiri umeendela kukua kutokana na mapinduzi ya viwanda na maboresho ya teknolojia kwa ajili ya kuzalisha bidhaa kwa wingi kwa kutumia mashine, na hivyo, kupunguza pia ajira kwa kazi zilizokuwa zikifanywa kwa mikono kwani haikuwa tena na sababu.

Laborem Exercens ilichapishwa mnamo tarehe 14 Septemba 1981, kwanza kabisa kwa lengo la kuadhimisha miaka 90 ya waraka wa kwanza wa kijamii ulioandikwa na papa Leo XIII, Rerum Novarum, mnamo mwaka 1891, ambao mapapa wote waliofuata waliendelea na wanaendelea kuutumia kama rejea katika kuendeleza mafundisho jamii ya Kanisa. Pili, Laborem Exercens iliandikwa kwa ajili ya kukabiliana na mabadiliko makubwa ya kijamii yaliyoikumba dunia tangu Mapinduzi ya Viwanda yalipotokea katika nchi za Ulaya na Marekani, mapinduzi ambayo yalileta pia athari kwenye uelewa wa hadhi na haki za wafanyakazi.

Papa Yohane Paulo II anabainisha baadhi ya mabadiliko haya na athari zake katika ulimwengu wa ajira na, mabadiliko ambayo yalihitaji marekebisho kwenye miundo ya uchumi na utoaji wa ajira.Mabadiliko haya yanahusu: maendeleo ya sayansi na teknolojia na ueneaji wa mashine za kuzalishia bidhaa viwandani, kuongezeka kwa gharama za nishati na malighafi, uhaba wa rasilimali ya dunia, na uelewa juu ya uharibifu wa mazingira. Vile vile, LE iliandikwa kwa ajili ya kukabiliana na uelewa hasi juu ya maana ya kazi na upungufu wa maadili katika ulimwengu mamboleo.

Katika kuongelea swala la kazi, mwanadamu anapewa kipaumbele cha pekee kwani kazi inayo hadhi yake, na hadhi hiyo inatokana na kwamba kazi inafanywa na mwandamu. Katika waraka huu, papa yohane Paulo II anasisistiza kwamba, kwa njia ya kufanya kazi, au kwa njia ya kazi, mwanadamu anaendeleza kazi ya uumbaji ambao tayari Mungu aliuanza. Kwa hiyo, kadiri ya mafundisho ya papa juu ya kazi, ni kwamba kitu cha kuthamini si kazi kama kazi bali ni mwanadamu anayefanya kazi na ambaye anaipatia maana kwa utu na utendaji wake. Vilevile , kazi inampatia mtu hadhi katika maana kwamba, pale mtu anapofanya kazi na kuzalisha, anaweza kukidhi mahitaji yake binafsi na mahitaji ya wale ambao wako chini ya ulinzi na usimamizi wake.

Mambo yanapofanyika kinyume na hivi, matokeo yake ni mtu kuchukuliwa kama mojawapo ya vyombo vya kuzalishia faida inayotokana na kazi, au hata kuuzwa kama bidhaa. Hali hii ina kuudhalilisha utu wa mtu, jambo ambalo halikubaliki machoni pa mwenyezi Mungu. Ili kuweza kuondokana na nayanyaso ambazo wafanyakazi wanaweza kukumbana nazo, papa anatoa ushauri kwamba wafanyakazi waunde vyama vya ushirika wa wafanyakazi ili kwa pamoja na kwa mshikamano waweze kuwa na nguvu ya kudai haki zao ambapo haziheshimiwi. Vyama hivi, kadiri ya mafundisho ya Papa Yohane Paulo II vitasaidia pia katika kupata haki katika jamii.

Kanisa Katoliki katika Mafundisho yake Jamii daima limetoa kipaumbele cha pekee kwa mwanadamu. Kutokana na ukweli kwamba kazi ni tendo linalo pata chumbuko katika utashi wa mwanadamu, kinachofuata ni kwamba, mwanadamu anashiriki katika kazi kwa hali zake zote kiroho na kimwili. Kwa maana hiyo, Kanisa linao wajibu na jukumu la kuwaelewesha watu kuhusu thamani ya kazi na maadili yanayopaswa kuambatana nayo na kwa njia hii kuonesha taalimungu iliyopo kwenye kazi. kusema kwamba kazi pia inayo tasaufi yake ina maanisha kwamba kwa njia ya kufanya kazi kwa uadilifu mwanadamu anaweza pia kuishi katika muunganiko na Mungu na kukuza urafiki na Yesu Kristo mkombozi wa dunia, na hivi kuendeleza ule mpango wa ukombozi ulioletwa na Mungu mwenyewe. Papa Yohane Paulo II katika waraka huu anashauri kwamba maisha ya kiroho hayahusu tu sala, tafakari, kusifu na kuabudu, au mambo mengine kama hayo, bali pia maisha ya kiroho yanaweza kuhusisha pia kazi.

Hapa ina maanisha kwamba, ikiwa mtu katika utendaji wake wa kazi yoyote halali, anaifanya si tu kwa ajili ya manufaa yake mwenyewe bali pia kwa ajili ya kuwasaidia wengine na kwa nia ya kuendeleza kazi ya uumbaji wa Mungu, hata hapa kuna uhusiano kati ya kazi na maisha ya kiroho.

Waraka huu unatoa mtizamo mpy wa maisha ya kiroho na unatualika sote tuondokane na ile dhana ya kuelewa maisha ya kiroho kama hali ya kujikatalia na kuenzi dhana nyingine ambayo ni maisha ya kiroho yanayo mfanya mtu awajibike mbele ya jamii na kwenye jamii, bila kuaiacha safari yake ya kiroho. Kazi ni wito ambao mwanadamu ameitiwa tangu kuumbwa kwa ulimwengu, pale Mungu alipomwambia Adamu kwamba atapata chakula chake kwa njia ya jasho la uso wake, yaani kwa njia ya kazi.

Kupata chakula kwa njia ya jasho kuna maanisha kuchoka, na hata kupoteza nguvu za mwili kwa namna moja au nyingine, na hii inaweza kuonekana kama sehemu hasi ya kazi. sehemu chanya ni ile inayotokana na kwamba, kwa njia ya kazi mwanadamu anashiriki kazi ya uumbaji na anaiendeleza, na kwa kuiendeleza anajipatia pia kipato chake kinachomfanya aishi katika maisha yenye hadhi kwenye jamii na kuwawezesha wengine kuishi maisha yenye hadhi. Ila hata katika sehemu hasi ya kazi, ambayo ni mchoko, Papa Yohane Paulo II alitufundisha kuipa thamani. Anasema, uchovu na shida zinazotokana na kazi vinaweza kuwa na thamani ikiwa mwanadamu, na hasa mkristo, ataviunganisha na mateso ya Kristo.

Papa anafundisha kwamba “ kwa njia ya uvumillvu wa uchovu unaotokana na kazi, na kwa kuunganisha uchovu huo na mateso ya Kristo aliyesulibiwa kwa ajili yetu, mwanadamu anashirikiana na mwana wa Mungu katika kazi ya kuuokomboa ulimwengu. Hivyo basi, kwa namna hii tunaweza kusema kwamba, mafundisho ya Papa Yohane Paulo II kuhusu kazi ni kwamba, kwa njia ya kazi mwanadamu anashirki katika uumbaji na ukombozi wa ulimwengu.
Imeandaliwa na Sr. Gisela Upendo Msuya,
Chuo Kikuu cha Kipapa cha Mtakatifu Toma wa Akwino,
Angelicum, Roma.








All the contents on this site are copyrighted ©.