2014-04-22 12:08:31

Wanawake simameni kidete kutetea Injili ya Uhai, msikubali kukumbatia utamaduni wa kifo!


Kardinali Polycarp Pengo, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Dar es Salaam anawahamasisha wanawake kuwa ni watetezi wakuu wa Injili ya uhai badala ya kukumbatia utamaduni wa kifo, unaojikita katika sera za utoaji mimba na mpango wa uzazi, unaowanyima watoto fursa ya kuzaliwa kwenye familia. Kardinali Pengo amewataka wanawake na wasichana kukuza dhamiri nyofu kwa kuheshimu Amri za Mungu na Mafundisho Kanisa.

Kardinali Pengo ameyasema hayo, wakati wa Ibada ya Misa Takatifu, Jumatatu ya Pasaka, iliyowaunganisha waimbaji wa Shirikisho la Kwaya Jimbo Kuu la Dar es Salaamili kusherehekea Siku kuu ya Pasaka pamoja. Wanawake wana nafasi kubwa katika kuleta mabadiliko ndani ya Jamii, kwa kulinda na kudumisha misingi ya haki, amani na utulivu, kumbe kuna haja kwa wanawake na wasichana kufundwa sawasawa, ili waweze kuwa na dhamiri nyofu, itakayowasaidia kusimama kidete kulinda na kutetea Injili ya Uhai, tangu pale mtoto anapotungwa mimba tumboni mwa mama yake hadi mauti ya kawaida inapomfika kadiri ya mpango wa Mungu

Kardinali Polycarp Pengo amekemea pia tabia ya baadhi ya watu kudai haki ya kuwa na ndoa za watu wa jinsia moja, kwamba ni jambo linalokiuka Amri za Mungu, maadili na utu wema.







All the contents on this site are copyrighted ©.