2014-04-20 09:55:45

Zawadi ya Pasaka kutoka kwa Papa Francisko kwa maskini wa mji wa Roma!


Askofu mkuu Konrad Krajewski,Mtunza sadaka ya Papa katika maadhimisho ya Siku kuu ya Pasaka kwa Mwaka 2014 amewatembelea maskini wa mji wa Roma na kuwapatia zawadi ya Pasaka kutoka kwa Baba Mtakatifu Francisko. Hawa ni watu wanaoishi katika maeneo ya vituo vikuu vya reli, eneo la Kanisa kuu la Bikira Maria mkuu mjini Roma pamoja na Ostiense.

Zawadi ya Baba Mtakatifu kwa maskini ni mchango unaotolewa na waamini pamoja na watu wenye mapenzi mema wanapoomba vyeti vya baraka kutoka kwa Baba Mtakatifu. Zawadi na ukarimu wa Baba Mtakatifu Francisko katika kipindi hiki cha Kwaresima imewafikia pia wanawake 30 wanaotunzwa na Masista wa Mama Theresa wa Calcutta.

Askofu mkuu Krajewski anasema, Baba Mtakatifu Francisko alipomteuwa kuwa Askofu mkuu na mtunza sadaka wake, alimtaka kumsaidia kuwafariji maskini na kamwe asijenge mazoea ya kukaa ofisini na kwamba, mahubiri ya Padre Raniero Cantalamessa, mhubiri wa nyumba ya Kipapa amekazia umuhimu wa kutumia fedha kwa busara na kamwe watu wasitawaliwe na uchu wa mali kwani matokeo yake ni mabaya katika maisha ya watu.







All the contents on this site are copyrighted ©.