Ujumbe wa kichungaji kwa Pasaka kutoka Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania
Ufuatao ni Ujumbe wa kichungaji wa Pasaka 2014 kwa waamini na Watu wote wenye mapenzi
mema unaoongozwa na kauli mbiu “sote tuwe na umoja” (rej. Yn 17:21) kutoka kwa Baraza
la Maaskofu Katoliki Tanzania.
UTANGULIZI:
Ndugu wapendwa, tunapohitimisha kipindi cha Kwaresima kilichokuwa na ujumbe: “Ukweli
utawaweka huru” (Yn. 8: 32), tunawaletea ujumbe wa “Umoja” ili kuongeza msisitizo
kwenye ujumbe wetu wa Kwaresima. Tunaitwa kukubali kuwa umoja ni ukweli msingi wa
kila mafanikio ya jumuiya ya mwanadamu. Ufufuko ni Pasaka inayomaanisha kivuko
au kupita kwa Wayahudi toka kwenye matatizo ya utumwa hadi uhuru kamili. Kwa Wakristo
ni kuvuka kutoka utumwa wa fikra za kifo (dhambi) hadi uhuru kamili wa ufufuko wetu
na Bwana Yesu. Kwahiyo, furaha za Pasaka zinapaswa kusheheni shukurani za dhati kwa
zawadi nyingi alizotujalia Mungu Muumba wetu tokea mwanzo na hasa nyakati hizi katika
mwanga wa Ufufuko wa Kristo. Adhimisho la Pasaka litawaliwe na furaha, amani na matumaini
makuu yaliyoletwa kwa Ufufuko wa Bwana wetu Yesu Kristo. Mtume Paulo anatuambia: “Mungu
na ashukuriwe atupaye kushinda kwa Bwana wetu Yesu Kristo” (1Kor. 15:57). Wakati
dhambi na kifo husababisha kujitenga; uhuru, furaha na amani husababisha kuungana.
Ndivyo ilivyotokea kwa Adamu na Eva. Walipokuwa bila dhambi walikuwa huru, wenye furaha,
amani na umoja na Mungu. Walipotenda dhambi walimkimbia Mungu, wakatafuta kujificha.
Hata wao wenyewe walioneana aibu na hatimaye wakafukuzwa kutoka kwenye bustani ya
Edeni (Mwa. 2:25; 3:7-8, 23-24).
1. Ndugu zetu katika Kristo, “Amani iwe Kwenu”
(Yn. 20:19). Wakati huu wa Pasaka, wakati ambao pia mchakato wa kuandika Katiba ya
nchi yetu unaendelea, hatuwezi kuacha kutafakari kwa dhati juu ya umoja wetu sisi
Watanzania. Bila shaka, moja ya mihimili mikubwa ya umoja wa kitaifa ni uongozi bora.
Mwenyezi Mungu aliwatoa watu wake utumwani Misri na kuwaweka huru kwa kuwateulia
viongozi miongoni mwao. Kiongozi wa kwanza alikuwa Musa (Kut. 3:10).
Chini
ya uongozi wa Musa Wayahudi walichukua muda mrefu kujenga umoja na uelewa, kwamba
walikuwa watu wa Mungu na walipaswa kumtambua kiongozi wao kama mteule wa Mungu (Kut.
16:3; 17:4;). Katika kutangatanga kwao jangwani, iliwachukua pia muda mrefu kutambua
uovu wao na kujitakasa dhidi ya dhambi zao (Kut. 32:1-14). Hata wakiwa tayari
katika nchi waliyoahidiwa hawakuacha machukizo yao kwa Mungu pamoja na kukanywa mara
kwa mara na Manabii wake Mwenyezi Mungu (Amu. 2:11-13).
Wakati ulipowadia,
Mungu alimtuma Mwanae Yesu Kristo kujenga Utawala wa Mungu juu ya msingi wa imani
na ukweli (Gal. 4:4):
Imani kwa Mungu na imani baina ya watu wenyewe
– kuaminiana – ndio msingi wa Utawala wa Mungu (2Thes. 2:13-17). Lakini kutokana
na udhaifu wa kibinadamu, mara nyingi tunavunja umoja wetu na Mungu na kati yetu wenyewe
kwa kiwango cha kutotaka kuishi pamoja; tunabaguana na hatutendeani haki (Mwa. 4:7-8).
Katika
ulimwengu wa leo, tunashuhudia madhara ya utengano wa namna nyingi. Dhambi nyingi
za binadamu zinasababisha mifarakano na vita. Hayo ni matukio ya kila mara katika
nchi nyingi ulimwenguni na hasa kwetu Afrika. Hata historia yetu wenyewe ina matukio
mengi ya jamii kufarakana na kujizamisha katika vita.
Mababu
zetu walipitia maisha marefu ya kuhamahama na kuchukuliwa utumwani na wengine kubaki
watwana na watawaliwa wa kikoloni kwa vipindi virefu kabla ya kujipatia uhuru wa kujitawala. Tulipopata
uhuru, tulijifunza kujenga umoja katika tofauti zetu kubwa za kikabila na kufikia
taifa moja. Tulichukua hatua kubwa kuunganisha nchi mbili huru, Tanganyika na Zanzibar,
na kuifanya kuwa nchi moja ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ikiwa kielelezo kwa
Bara la Afrika cha kujenga umoja.
2. Hatua zote hizo tulizopitia na
tulizochukua kwa makusudi kabisa, tulikuwa na nia na utashi wa kuwa wamoja. Tulitaka
kujenga maendeleo ya pamoja na mafanikio ya kila Mtanzania kufikia maisha bora. Jitihada
hizi njema zimekuwepo kwa miaka hamsini iliyopita. Tumefanikisha mambo mengi katika
umoja wetu ambao unatusukuma kumshukuru Mungu. Kwa muda mrefu umoja wa Watanzania
umeonekana kwa mataifa mengine kuwa ni kielelezo cha umoja wa kitaifa wa hali ya juu
sana. Ni umoja uliokua kufikia kiasi cha kufuta tofauti za awali za mataifa yaliyohusika
kuunda umoja. Tunamshukru mwenyezi Mungu kwa kuifanya Nchi yetu kuwa kimbilio
la waliokata tamaa. Tanzania imewapa wakimbizi mahali salama pa kuishi pamoja na Watanzania.
Chini ya Jamhuhuri ya Muungano wa Tanzania, waliokuwa bado chini ya wakoloni, waliandaliwa
kujikomboa na kuwa mataifa huru. Pamoja na mafanikio hayo makubwa, zimejitokeza
dosari kadhaa katika umoja zilizofanya umoja wetu upoteze baadhi ya sifa zake za awali.
Kupungua kwa hisia za kujisikia watu wote ni taifa moja, ni dosari iliyoanza kukua
taratibu na sasa inaonekana kuwa ndio ukweli. Baadhi ya Watanzania wanafikiri kuwa
umoja unaofuta tofauti haufai ila umoja unaosisitiza tofauti kama ulivyo umoja wa
kikanda (kama ilivyo SADC, ECOWAS, n.k) ndio unafaa! Wakati mataifa mengine yanatamani
umoja unaofanana na ule umoja wetu wa awali, baadhi yetu tunatamani kurudi nyuma kwenye
umoja wa mpito! Kutokana na mapungufu yaliyodhihirika ndani ya mafanikio yetu,
umuhimu wa kufanya marekebisho ulidhihirika. Ni kwa sababu hiyo, watu wengi walitaka
na wanataka mabadiliko au mageuzi ya msingi sana. Kwa msukumo huo ndio sababu tuliingia
katika mchakato wa kuandika Katiba Mpya. 3. Kazi ya kuandika Katiba si nyepesi
na yataka umakini mkubwa. Haishangazi sana tunapojionea mivutano na migongano ya hoja
kutoka kwa makundi kinzani katika nchi moja. Mawazo ya wengi yamewasilishwa kisheria
na Tume ya Mabadiliko ya Katiba kwa ajili ya kujadaliwa na Bunge Maalum la Katiba
(BMK). Sasa, tunashuhudia makundi yenye nguvu yakijaribu kushinikiza kuingizwa matakwa
yake kwenye Katiba kwa njia zozote zile ili kujihakikishia kuendelea kulinda maslahi
yake ya kisiasa. Wajumbe wa Bunge Maalum Katiba wanazozana, wanakashifiana,wanatukanana
na hawataki kuachana na itikadi za kisiasa ili kufikia muafaka katika masuala muhimu
yatakayowahakikishia raia wa kawaida kushiriki kwenye fursa za maendeleo kwa manufaa
ya wote. Hayo lakini yasitukatishe tamaa na kujiona kama tu watu wa kushindwa wakati
tukiwa bado kwenye mchakato mrefu wa kujipatia jukwaa jipya kwa mustakabali wa taifa
letu Tanzania. Tushirikiane na wote wenye nia njema kupambana na nguvu za maovu
na ubinafsi na kuachana na itikadi za kisiasa na matakwa ya kiuchumi ya matabaka ya
walio nacho ili kupigania haki za wanyonge. Tuandae Katiba ambayo itatupatia misingi
imara ya maadili itakayotuongoza kupigana dhidi ya ubinafsi na ufisadi, na kutetea
haki za binadamu kwa wote. Vigezo vyote muhimu kwa maisha ya mshikamano kitaifa vimeandikwa
katika Rasimu ya Katiba Sura ya 1 hadi ya 5. Tukisha kukubaliana na yaliyomo katika
sura hizo, muundo wowote wa Serikali unawezekana kwa kuzingatia kanuni za uwiano wa
madaraka na wajibu wa mihimili mitatu ya Dola kwa mujibu wa Sura za 8 hadi 15. Ili
tufikie lengo letu la kuwa na Katiba bora katika hatua tuliyofikia ya mchakato wa
Katiba Mpya yatubidi kuzingatia yafuatayo:
Kuheshimu kazi ya Tume
ya Mabadiliko ya Katiba na kuitumia kama ilivyokusudiwa na sheria iliyoiweka. Kuwa
na nia njema ya kweli ya kutafuta suluhisho la matatizo mengi ya utendaji katika Dola
zilizopo katika Muungano. Kuwa na hamu ya kujitoa kwa taifa na kulitumikia kwa
moyo bila kutawaliwa na ubinafsi au kujipendelea kiinchi na kiukanda kwa madhumuni
ya kuboresha maisha ya Watanzania wote. Chaguo la muundo wa Dola, sharti liongozwe
na malengo na madhumuni ya umoja wetu wa kutaka tuishi kwa mshikamano wa dhati. Uchaguzi
wa muuungano wa serikali moja, mbili au tatu sharti ufanywe kwa dhamiri safi iliyo
na uelewa uliochambua matatizo yaliyopo ya Muungano na kuridhia mfumo utakaosuluhisha
matatizo hayo pasipo mashaka yoyote.
4. Baada ya kutafakari historia
ya ukombozi wa mwanadamu kwa ufupi na hatua Watanzania tuliyofikia katika uhuru wetu
wakati huu wa adhimisho la Ufufuko wa Bwana wetu Yesu Kristo mwaka 2014, tungependa
kwa namna ya pekee kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kumvuvia Rais Jakaya M. Kikwete ujasiri
wa kuamua kuanzisha mchakato wa kuandika Katiba Mpya ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
kisheria katika wakati muafaka. Kwa mchakato huo wa Katiba, kupitia Tume yake Huru,
Watanzania wamepata fursa ya kusema kila jambo lililowaelemea maishani na kuainisha
namna wanavyotaka kujitawala. Wakati ulikuwa mwafaka kwa sababu kulikuwa na manung’uniko
mengi ya ukiukwaji wa Katiba ya sasa ambayo hayakuweza kujibiwa na Serikali zilizopo.
Hatua ya kuamua kuyakabili hayo kwa sheria ya Kurekebisha Katiba iliwapa wananchi
fursa ya kutoa maoni yao bila mizozo na machafuko.
5. Tume ya Mabadiliko ya
Katiba imewasilisha kwenye Bunge Maalum la Katiba Rasimu ya Katiba iliyotokana na
maoni huru ya watu binafsi na makundi mbali mbali zikiwemo taasisi za dini, mamlaka
za kiserikali na asasi huru za kiraia. Tunalisihi na kulishauri Bunge Maalum la Katiba
kuheshimu mawazo yaliyowasilishwa na kutumia busara zilizopendekezwa za kujenga muundo
wa Muungano utakaokidhi mahitaji ya utangamano, mshikamano, amani, maadili, uhuru
na uwajibikaji wa viongozi na raia wa Tanzania.
HITIMISHO
Ndugu wapendwa,
Wakati huu wa Pasaka, tuendelee kuliombea Bunge Maalumu la Katiba ili wajumbe
wawe wazingatifu wa matakwa na matarajio ya Watanzania yalivyoainishwa katika Rasimu
ya Pili ya Katiba na Tume ya mabadiliko ya Katiba kwa kuheshimu maoni ya Watanzania
na kuboresha maoni hayo kwa hekima na busara ili kulinda mstakabali wa Taifa letu;
Tanzania yenye amani kwa ustawi wa watu wote.
Tuombe: Ee Bwana, katika
upendo wako uwape neema watu wa taifa lako, waishio Tanzania. Katika upendo wako ujenge
tena nguzo za imani, matumaini na mapendo katika mji nchi yetu. Watanzania wakiwa
na imani, matumaini na mapendo ya haki utapendezwa na sadaka wakutoleazo; kila mtu
akijitolea yeye mwenyewe kwako kama sadaka safi juu ya altare, pamoja na katika Kristo
Mfufuka aliye katika Ekaristi. Mama Bikira Maria atuombee ili ndani yetu uzaliwe
upya uaminifu unaotupa uwezo wa kutangaza kazi kuu ya Mungu. Tunaomba hayo kwa njia
ya Kristo Bwana wetu. Amina.
Amani ya Kristo Mfufuka iwe nanyi
Ni sisi
Maaskofu wenu: Mhashamu Askofu Tarcisius Ngalalekumtwa, Rais wa Baraza la Maaskofu
Katoliki Tanzania, Askofu wa Iringa Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo, Dar es
Salaam Mhashamu Askofu Mkuu Josaphat Lebulu, Arusha Mhashamu Askofu Mkuu Paul
Ruzoka, Tabora/Kigoma Msimamizi Mhashamu Askofu Telesphor Mkude, Morogoro Mhashamu
Askofu Gabriel Mmole, Mtwara Mhashamu Askofu Mkuu Yuda Thaddaeus Ruwa’ichi, Ofm
Cap, Mwanza,/Shinyanga Mhashamu Askofu Bruno Ngonyani, Lindi Mhashamu Askofu
Anthony Banzi, Tanga Mhashamu Askofu Agapiti Ndorobo, Mahenge Mhashamu Askofu
Evaristo Chengula, IMC, Mbeya Mhashamu Askofu Augustino Shao, Cssp, Zanzibar Mhashamu
Askofu Damian Kyaruzi, Sumbawanga Mhashamu Askofu Severine NiweMugizi, Rulenge-Ngara Mhashamu
Askofu Desiderius Rwoma, Bukoba /Singida Msimamizi Mhashamu Askofu Method Kilaini,
Bukoba Mhashamu Askofu Damian Dallu, Geita/Askofu Mkuu Mteule Songea Mhashamu
Askofu Ludovick Minde, OSS, Kahama Mhashamu Askofu Alfred Leonard Maluma, Njombe Mhashamu
Askofu Castor Paul Msemwa, Tunduru-Masasi Mhashamu Askofu Beatus Kinyaiya, Ofm
Cap, Mbulu Mhashamu Askofu Michael Msonganzila, Musoma Mhashamu Askofu Issac
Amani, Moshi Mhashamu Askofu Almachius Rweyongeza, Kayanga Mhashamu Askofu
Rogath Kimaryo, Same Mhashamu Askofu Salutaris Libena, Ifakara Mhashamu Askofu
Eusebius Nzigilwa, Dar es Salaam Mhashamu Askofu Renatus Nkwande, Bunda Mhashamu
Askofu Gervas Nyaisonga, Mpanda /Dodoma Mhashamu Askofu Bernadin Mfumbusa, Kondoa Mhashamu
Askofu John Ndimbo, Mbinga Mhashamu Askofu Titus Mdoe, Dar es Salaam