2014-04-20 09:27:13

Msalaba wa Kristo unafumbata: upendo, huruma na msamaha!


Ibada ya Njia ya Msalaba kuzunguka magofu ya Colosseo wakati wa Ijumaa kuu, ilikuwa ni nafasi kwa Mama Kanisa kuangalia sura ya Kristo katika mateso na mahangaiko ya watu wake. Baba Mtakatifu Francisko mara baada ya maadhimisho ya Njia ya Msalaba alisema kwamba, Yesu amebeba dhambi za binadamu katika mabega yake na kwamba, usaliti wa Yuda na Petro uliongeza uzito wa Msalaba. Huu ndio uzito wa Msalaba unaojionesha kwa watu wanaoishi katika upweke hasi, dalili za kifo; kifo kwa ndugu na jamaa pamoja na uwepo wa dhambi!

Msalaba ni kielelezo cha upendo, utukufu na huruma ya Mungu kwa binadamu ambaye kamwe, hawatendei watu wake kadiri ya dhambi zao, lakini kadiri ya huruma na upendo wake. Kwa njia ya mateso ya Kristo Msalabani, mwanadamu anaonja upendo wa Kristo na tumaini la maisha mapya.

Mwanadamu daima yuko katika hija ya maisha ambayo hatima yake ni kifo, lakini kwa njia ya Fumbo la Pasaka, Yesu ameshinda kifo na dhambi na kwamba, upendo, huruma na msamaha wa Mungu ni mambo msingi katika hija ya maisha ya mwanadamu. Baba Mtakatifu anawaalika waamini kumkimbilia Kristo katika mateso yake, ili waweze kufufuka pamoja naye.







All the contents on this site are copyrighted ©.