Wachunguzi wa mambo ya kisiasa wanasema kwamba, hali ya kisiasa nchini Burundi kwa
sasa ni tete kutokana na mpasuko pamoja na kinzani za kisiasa na kikabila zinazoendelea
kujionesha siku hadi siku, kiasi hata cha kutishia amani, ustawi na maendeleo ya wananchi
wa Burundi. Rais Pierre Nkurunziza ameanza kujielekeza katika mchakato wa marekebisho
ya Katiba ili kumpatia nafasi ya kuwania tena Urais kwa kipindi cha tatu mfululizo
kinyume cha Katiba ya Burundi.
Taarifa ya siri iliyokuwa imeandaliwa kwa ajili
ya Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa inaonesha kwamba, Serikali ya Burundi ilikuwa imewapatia
silaha wanajeshi wa Chama tawala. Haya ni mambo ambayo yameichefua Serikali ya Burundi
kiasi hata cha kumfukuza Bwana Parfait Onanga-Anyanga, Mwakilishi wa Umoja wa Mataifa
nchini Burundi. Kwa mwelekeo huu, kuna hatari ya kuweza kuzuka tena kwa vita ya kimbari,
kama ilivyowahi kujitokeza nchini humo, miaka ishirini iliyopita!