Askofu mkuu Paulo Ruzoka, Mwenyekiti wa Tume ya haki na amani ya Baraza la Maaskofu
Katoliki Tanzania katika mahojiano maalum na Radio Vatican, wakati wa Maadhimisho
ya Ijumaa kuu anasema, hii ni siku ambayo Mama Kanisa anakumbuka mateso na kifo cha
Kristo Msalabani.
Ni siku ya
majonzi na simanzi inazomwonesha Yesu aliyejisadaka kwa ajili ya wokovu wa walimweng
pamoja na kutimiza mapenzi ya Baba yake wa mbinguni. Lengo lilikuwa ni kuwatangazia
watu Habari Njema ya Wokovu inayomwonesha Mungu ambaye ni mwingi wa huruma na mapendo
kwa wote.
Askofu mkuu Ruzoka anasema hakuna mateso makali zaidi kuliko kutengwa
na Mwenyezi Mungu, kwani huku ni sawa na kuishi gizani pasi na mwanga wa imani, matumaini
na mapendo. Kwa mateso, kifo na ufufuko, Yesu ameleta mwanga, hali na mwelekeo mpya
na hivyo wote wamefanyika kuwa ni watoto wateule wa Mungu. Kumbe, maadhimisho ya Ijumaa
kuu ni msingi mkuu wa tumaini la Pasaka, chemchemi ya furaha, amani, upendo na mshikamano.
Huu ni mlango mpya katika maisha ya mwanadamu, kwani Yesu anawakomboa watu
kutoka katika giza la kukosa mwanga wa imani na ufahamu na hatimaye kuwakirimia maisha
mapya katika haki na ukweli. Ijumaa kuu ni msingi wa tumaini na hatima ya mwanadamu
katika mchakato wa kufikia maisha ya uzima wa milele.
Askofu mkuu Ruzoka anasema
kwamba, watanzania wako katika mchakato wa kuandika Katiba Mpya, inayohitaji umakini
mkubwa katika kujenga na kuimarisha mshikamano wa kitaifa. Watanzania wanangojea kwa
matumaini makubwa kupata Katiba Mpya itakayowawezesha kuondokana na mambo yanayokwenda
kinyume cha maisha ya binadamu; mambo ambayo kimsingi yanavuruga: haki, amani na utulivu;
kwa kuwajaza watu hofu pamoja na mashaka ya hatima ya maisha yao.
Askofu mkuu
Ruzoka anasema, watanzania wanapaswa kujiaminisha kwa Kristo Yesu, ili aweze kuwanusuru
katika mambo yote haya. Mchakato wa Katiba Mpya nchini Tanzania unawanyima watu wengi
usingizi. Watanzania wanaendelea kujiuliza maswali ya msingi, Je, Tanzania itapata
Katiba Mpya itakayofuta machozi na mahangaiko ya watanzania wengi? Je, itakuwa ni
Katiba inayoleta: mwanga, mwono, dira na mwelekeo mpya katika medani mbali mbali za
maisha ya mtanzania?.
Askofu mkuu Ruzoka anasema, kuandika Katiba Mpya ni kazi
nyeti na tete. Kumbe, kuna haja kwa waamini na watu wote wenye mapenzi mema kuwasindikiza
wabunge wa Bunge Maalum la Katiba kwa njia ya sala na majitoleo, ili kweli Katiba
Mpya ambayo ni sheria mama iweze kuwaweka watanzania wote huru; kwa kujenga na kuimarisha
umoja na mshikamano wa kitaifa; kwa kuheshimu na kuzingatia utawala bora.
Waamini
waendelee kuwaombea wabunge kwa Mwenyezi Mungu ili aweze kuwaangazia akili zao na
kuimarisha utashi wao ili waweze kutekeza dhamana hii nyeti kwa ajili ya mafao ya
watanzania wengi ili kuwapatia watanzania Katiba Mpya ambayo italinda na kudumisha
maendeleo ya sasa na kwa ajili ya vizazi vijavyo.
Imeandaliwa na Padre Richard
A. Mjigwa, C.PP.S. Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.