2014-04-15 07:47:26

Mchango wa waamini walei katika maandalizi ya mkutano mkuu wa AMECEA


Askofu mkuu Tarcisio Ziyaye, Mwenyekiti wa Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Afrika Mashariki na Kati, AMECEA, hivi karibuni amezindua kamati ya waamini walei 75 kutoka Jimbo kuu la Lilongwe, Malawi, kusaidia mchakato wa maandalizi ya maadhimisho ya mkutano mkuu wa AMECEA unaotarajiwa kufanyika mjini Lilongwe, Malawi kuanzia tarehe 14 hadi tarehe 26 Julai 2014. RealAudioMP3

Kamati hii inaundwa na wajumbe walioteuliwa kutoka katika Parokia mbali mbali za Jimbo kuu la Lilongwe kutokana na ujuzi, weledi na majitoleo yao katika maisha na utume wa Kanisa nchini Malawi. Askofu mkuu Ziyaye amewashukuru na kuwapongeza waamini nchini Malawi kwa kujitokeza kwa wingi pamoja na kuonesha nia ya kuchangia kwa hali na mali ili kufanikisha maadhimisho ya mkutano wa AMECEA.

Kamati hii ya watu 75, itashirikiana na Kamati nyingine ya watu 20 iliyokuwa imeundwa mwaka 2012 kwa ajili ya maandalizi ya awali, hususan katika kutafuta fedha za kugharimia mkutano wa AMECEA. Kundi hili kwa sasa limegawanyika katika kamati ndogo ndogo za: chakula, malazi, ulinzi na usalama, matangazo, afya na protokali. Askofu mkuu Ziyaye amewataka waamini wanaotaka kutolea muda wao kwa ajili ya kuwahudumia wajumbe wa mkutano wa AMECEA kujiandikisha mapema Jimboni Lilongwe, kwani watu wengi zaidi watahitajika kwa ajili ya kutoa huduma.

Mkutano mkuu wa AMECEA kwa Mwaka 2014 unatarajiwa kuhudhuriwa na wajumbe 300 kutoka katika nchi zinazounda AMECEA pamoja na wageni waalikwa. Hili ni tukio la Kikanisa litakalotoa nafasi kwa Familia ya Mungu katika nchi za AMECEA kuweza kusali, kutafakari na kujadiliana masuala yanayogusa maisha na utume wa Kanisa katika nchi hizi.








All the contents on this site are copyrighted ©.