2014-04-14 09:16:19

Tujikumbushe yafuatayo katika Juma kuu!


Mpendwa msikilizaji wa Kipindi chetu cha Kanisa la Nyumbani, Tumsifu Yesu Kristo. Katika vipindi viwili vilivyopita, tulitafakari kwa uzito wa kutosha juu ya dhambi, toba, msamaha na kujirekebisha. Leo tunahitimisha tafakari zetu zile mbili kwa kuzipa muhutasari-unganifu. RealAudioMP3

Tunakubaliana kimsingi kwamba, mwanadamu ameumbwa kwa mwili, roho, akili na utashi. Katika makuzi ya mtu, ni vema hayo yote manne yakue sambamba. Endapo mwili peke yake utakuwa huku roho haikui, huyu mtu anakuwa mdumavu wa kiroho. Roho iliyodumaa ni hatari katika maisha. Mtu mdumavu kiroho hana uhusiano mzuri na ulimwengu wa mambo ya kiroho, haoni thamani ya Mungu katika maisha yake, haoni umuhimu wa sala na wala hafikiri maisha baada ya halafu. Yeye maisha yake yote yamejaa sasa, basi. Na kwa upande mwingine, endapo roho tu itakuwa na mwili utadumazwa, hiyo nayo ni hatari. Tushughulikie afya ya roho na mwili, ili kuwa na makuzi sambamba.

Pamoja na hayo, sisi wanadamu tumepewa akili na utashi. Kwa tafanusi nyepesi zinazosadifu tafakari yetu, tunaweza kutafsiri akili kama uwezo wa kujua/kutambua/kupembua kati ya jema na baya. Akili yetu inatusaidia kujua maana ya kitu au jambo na kupembua thamani yake huku tukihusisha na maisha yetu na maisha ya wenzetu. Utashi ni uwezo wa ndani wa kuamua. Kile ambacho akili inajua kuwa ni chema au kibaya, utashi sasa ndio hufanya kazi ya kuamua kutenda au kutotenda.

Katika haya mawili pia, AKILI na UTASHI ni vema viwe na makuzi sambamba. Tujibidishe kwa maumivu kabisa kukuza akili zetu kwa kujipatia maarifa mbalimbali yaliyo mema yenye kutujenga. Tunafanya hivyo kwa kujisomea maandiko matakatifu, kuongea na watu wenye hekima, kupata mafunzo mbalimbali ya maisha yetu nk. Tunaimarisha utashi wetu kwa kujenga dhamiri iliyo njema, dhamiri yenye hofu ya Mungu, na kuimarisha ujasiri ule wa kuamua kutenda au kutotenda lile ambalo akili yetu inalifahamu katika undani wake.

Maarifa hayo mepesi yatusaidie kuelewa kwa nini sisi wanadamu tunakuwa wepesi sana kurudi tena dhambini. Jibu hapo ni dhahiri, kwa wengine wetu ni kwa sababu ya kwashakoo ya roho, au kwashakoo ya akili, au utapiamlo wa utashi au vyote kabisa. Na tumeona jinsi ambavyo dhambi zinatutafuna na kutuangamiza katika maisha yetu ya kila siku! Tunatubu, lakini dakika chache baadaye tunarudi kulekule. Ni kwa nini? Tunajua tunachotenda? Lengo la kutubu lilikuwa ni nini? Tufanyeje ili walao tujitahidi tusiporomokee tena madhambini? Kuna machache ya kuyazingatia hapa.

La kwanza, tujue kwamba dhambi na maisha ya dhambi sio hulka ya mwanadamu. Mwanadamu ameumbwa kwa sura na mfano wa Mungu. Sehemu mmoja ya sura na mfano wa Mungu ni utakatifu wake. Sisi wanadamu tunashiriki katika utakatifu wa Mungu. Dhambi ni doa linalokuja juu ya utakatifu huo, hivyo huweza kuondoka na sisi tukabaki salama. Kwa neno hilo dogo, tuelewe kwamba, sisi wanadamu tunaweza kujibidisha kuwa mbali na dhambi, tukaikimbia na kuiacha kabisa.

Tatizo, wengi wetu tuna tabia ya kuikawaidisha dhambi. Ukiizoe dhambi na dhambi ikakuzoea, unaingia katika mtego wa kujirafikisha na dhambi, baadaye unaona ni kitu cha kawaida tu, na unaanza kufikiri na kujiaminisha kwamba ni vigumu kuishi bila kutenda dhambi. Hapana, hapo tunajidanganya. Mwanadamu hana undugu na dhambi, dhambi imekuja baadaye kama kupe na inaweza kuondoka na tukitaka haiji tena.

Pili, tukumbuke daima UBAYA wa dhambi na matokeo yake. Dhambi haina uzuri wowote, ni uangamizi tu, kama sio kwako mwenyewe basi kwa mwenzako, na kama sio leo basi kesho. Tunaposema tusiitamadunishe dhambi, tunataka kwa akili safi kukataa kabisa utamaduni wa dhambi, yaani kujiweka katika mazingira kwamba dhambi ni UTAMADUNI WETU. Sasa kwa leo hii, kutokana na matumizi mabaya ya akili yetu na utashi wetu, watu wengi tunatamadunisha dhambi, kwa kigezo cha haki za binadamu. Na hapo ndipo wanapoingia katika msigano na Kanisa. Hatuwezi kabisa kuhalalisha mifumo ya dhambi eti kwa kisingizio cha haki za binadamu.

Ni binadamu gani huyo mwenye HAKI ya kuangamizwa na dhambi? Ni katika hayo sauti ya Kanisa kama mama na mwalimu kwa watu wote na nyakati zote, itaendelea kusikika! Nani anaweza kuhalalisha mauaji ya watoto kwa njia za uuaji mimba eti ni HAKI ZA BINADAMU? Ni nani mwenye akili safi anayeruhusu kuchezacheza na sheria za kimungu mintarafu ndoa na familia, akalazimisha miungano ya jinsia moja kwa kigezo cha haki za binadamu? Je, haki ya mtoto anayeasiliwa na watu wa aina mmoja imezingatiwa? Ni nani mwenye haki ya kupanga haki ya mwenzake? Ni katika mazingira hayo ndiyo tunajikuta katika utamadunishaji wa dhambi, kwa maangamizi ya kizazi cha sasa na kijacho. Tunakwenda wapi?

Turudi kwenye misingi ya utu, haki ya kweli na uhuru wa waana wa Mungu. Tunajikabidhi kwa shetani kwa kujua na kutaka halafu tunadhani tutakuwa salama. Haiwezekani!! Kwa kila mtu binafsi, lazima kuwe na ile nguvu ya kiutashi ya kujipatia katazo lenye nguvu, kusema HAPANA KAVU mbele ya dhambi. Ni utashi wetu imara ndio utatusaidia tusiporomokee tena katika dhambi.

Tukiwa na utashi mtepetevu, daima tutajiangusha katika dhambi nyingi halafu baadaye tunatafuta namna ya kuzihalalisha ili ziwe haki za binadamu. Sema hapana kwa dhambi. Pamoja na hilo, lazima kuwa mwangalifu, usipende kujiweka katika mazingira ya dhambi au kujiambatanisha na makundi ya kidhambi au asasi zenye milengo-shetani ya waziwazi au iliyofichika.

Sisi kama jamii inayoishi sasa tunajiuliza swali mmoja, huu uangamizi tunaoufanya saa, ungetendwa na wazee wetu tungejikuta katika jamii ya aina gani duniani? Linaloonekana kwa nje ni kwamba jamii ya kimataifa haijibidishi kabisa kumdhamirisha mwanadamu katika kutambua ubaya wa UOVU na matokeo yake, badala yake inamhamasisha, inamlinda na kumsaidia mwanadamu kutenda madhambi zaidi, kwa kasi zaidi na kwa uhuru zaidi (kwa kigezo cha haki za binadamu). HAPANA, hapo mama Kanisa anasikitika, analia na kukataza kabisa. Tulinde, utu na uhuru wa kweli wa mwanadamu.

Sehemu ya mwisho tuone, ni nani anawajibika kwa dhambi za jamii? Kama tulivyokwisha kutafakari katika kipindi kilichopita juu ya aina ya dhambi, ni dhahiri kwamba kwa dhambi binafsi ni mwanadamu kila mmoja kwa nafsi yake anawajibika mintarafu toba. Kwa dhambi za jamii nani anawajibikia? Hapa tuseme tu kichungaji kwamba, ni mtu binafsi na jamii katika umoja inawajibika. Kama ilivyo dhambi binafsi, huvuruga uhusiano wetu na Mungu, hali kadhalika dhambi jamii huukorofi uhusiano wetu ndani ya jamii, tena huhaini uhusiano wetu na vizazi vijavyo na juu zaidi huharibu uhusiano wetu na Mungu. Kumbe jamii lazima ihusike.

Ni vema katika familia zetu katika mwaka, tuwe na siku mmoja ya kufanya toba kwa dhambi za familia. Kutafakari, kufunga na kutubu yale yote ambayo tumeghafiriana na kumkasirisha Bwana Mungu wetu. Pia katika jumuia ndogondogo, kigango, parokia, jimbo hata taifa tufanye hivyo.

Katika uangamizi wa familia ya mwanadamu huenda mimi na wewe tumeshiriki kwa namna fulani. Hatuwezi kunyamaza na kusema ‘ni hali ya kawaida tu’. Dhambi siyo hali ya kawaida, NI HALI YA HATARI.Tuikimbie dhambi, nasi tutakuwa salama. Kutoka katika Studio za Radio Vatican, ni mimi Padre Pambo Martin Mkorwe, OSB.








All the contents on this site are copyrighted ©.