2014-04-12 15:07:03

Yesu peke yake ndiye anayetoa maana ya kashfa ya mateso ya mtu mwadilifu!


Wajumbe wa kongamano la Chama cha Madaktari wa Upasuaji wa ugonjwa wa Saratani nchini Italia, lililoandaliwa na Chuo Kikuu cha La Sapienza mjini Roma na Hospitali ya ya Mtakatifu Andrea, Jumamosi, tarehe 12 Aprili 2014 walikutana na kuzungumza na Baba Mtakatifu Francisko mjini Vatican ambaye amewapongeza kwa huduma makini katika kuwahudumia wagonjwa.

Anasema, tafiti za kisayansi zimesaidia kwa kiasi kikubwa kuzuia, kutibu pamoja na kugundua tiba ya magonjwa mbali mbali. Madaktari ni watu wanaotekeleza dhamana kubwa na nyeti katika maisha ya watu, kwani wanapaswa kutoa majibu na matumaini kwa wagonjwa kutoka sehemu mbali mbali za dunia, changamoto ya kumthamini mwanadamu aliyeumbwa kwa sura na mfano wa Mungu; mwenye mwili na roho. Ugonjwa ni kielelezo cha maumivu na mateso ya mtu mzima na wala si sehemu tu ya mwili wake.

Baba Mtakatifu anasema kwa dhati kwamba, mwanadamu anahitaji kupata huduma makini ya tiba pamoja na kuonja mshikamano wa kibinadamu, kisaikolojia, kijamii na maisha ya kiroho pamoja na msaada kutoka kwa wanafamilia ya mgonjwa. Kutokana na ukweli huu, kuna haja kwa wahudumu katika sekta ya afya kuwa na mwono mpana kuhusu mwanadamu na kutoa mwelekeo wa kiutu kwa mgonjwa.

Baba Mtakatifu anawaalika kushirikiana kidugu na wagonjwa, ili kuwasaidia kugundua uzuri wa maisha hata katika hali tete, ili kutambua na kuenzi utu na heshima ya binadamu, tangu pale mtoto anapotungwa mimba tumboni mwa mama yake hadi mauti ya kawaida inapomfika kadiri ya mpango wa Mungu.

Baba Mtakatifu anawatakia wajumbe wote kheri na baraka tele katika maadhimisho ya Juma kuu litakalokamilika kwa mateso, kifo na ufufuko wa Yesu Kristo. Hapa Yesu aliweza kuumwilisha ubinadamu na uliokombolewa na Mwenyezi Mungu, ambaye ni chemchemi ya upendo. Yesu peke yake ndiye anayeweza kutoa maana ya kashfa ya mateso kwa mtu mwadilifu. Kristo aliyeteswa, akafa na kufufuka awe ni dira ya utekelezaji wa shughuli zao za kila siku.

Chini ya Msalaba, waamini wanapata fursa ya kukutana na Yesu pamoja na Mama yake anayeteseka. Huyu ni mama wa wote ambaye yuko daima karibu na watoto wake wagonjwa, akiwa na imani thabiti pasi na kutetereka. Baba Mtakatifu anawaombea kwa Bikira Maria ili aweze kuwasaidia katika tafiti na utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku.







All the contents on this site are copyrighted ©.