2014-04-11 16:14:11

Simameni kidete kupambana na utumwa mamboleo unaowanyanyasa watoto!


Chama cha Kimataifa cha Kutetea Watoto, BICE, kilianzishwa na kuridhiwa na Papa Pio wa kumi na mbili mara tu baada ya Vita kuu ya Pili ya Dunia, ili kulinda na kuwatetea watoto, harakati zilizochangia hata kuanzishwa kwa itifaki ya Umoja wa Mataifa kwa ajili ya watoto kunako mwaka 1989. BICE inaendeleza ushirikiano na Ubalozi wa Vatican kwenye ofisi za Umoja wa Mataifa.

Changamoto kubwa kwa sasa ni kusimama kidete kupambana na utumwa mamboleo unaowafanyisha watoto kazi za suluba, kuwanyanyasa pamoja na kuwadhulumu. Kuna haja ya kuhakikisha kwamba, watoto wanapata haki ya kuishi na kukua katika familia, wakiwa na wazazi wao wawili, yaani Baba na Mama, ili kuweza kufikia ukomavu katika mahusiano. Wazazi pia wanachangamotishwa kutekeleza wajibu wa kuwapatia watoto elimu inayojikita katika maadili, utu wema na maisha ya kiroho.

Ni changamoto iliyotolewa na Baba Mtakatifu Francisko wakati alipokutana na kuzungumza na wajumbe wa Chama cha Kimataifa cha kutetea watoto, waliomtembelea mjini Vatican, Ijumaa tarehe 11 Aprili 2014. Baba Mtakatifu anasikitika kusema kwamba, ikiwa kama watu wataendelea "kuchakachua" mifumo ya elimu, kuna hatari ya kukumbana na maafa kama ilivyojitokeza katika karne iliyopita kwa kuwasukumiza watoto na vijana kutembea katika "mawazo mgando".

Baba Mtakatifu anasema, kutetea haki msingi za binadamu kunahitaji majiundo makini ya kiutu kwa kumtambua binadamu na utu wake; kwa kujibu kikamilifu shida na changamoto anazokumbana nazo katika tamaduni mamboleo zinazoenezwa kwa kiasi kikubwa na vyombo vya upashanaji habari. Chama cha BICE hakina budi kujikita katika majiundo makini ya wanachama na wafanyakazi wake kuhusu utu na heshima ya watoto, kwani hapa ni kiini cha haki zao msingi na mipango yote ya elimu na malezi.







All the contents on this site are copyrighted ©.