2014-04-11 12:21:22

Mwenyeheri Yohane Paulo II mtetezi wa haki na amani


Haki na amani ni kati ya maneno makuu yaliyotumiwa na Mwenyeheri Yohane Paulo II katika maisha na utume wake kama Khalifa wa Mtakatifu Petro. Ni kiongozi aliyetoa hamasa kubwa kwa Jumuiya ya Kimataifa kupenda na kudumisha misingi ya haki na amani kwani amani ni tunda la haki na mapendo. RealAudioMP3

Amani ina msingi wake katika uelewa sahihi wa binadamu unaojikita katika katika haki na mapendo. Watu wanapaswa kujenga na kudumisha misingi ya haki na amani kwa njia ya majadiliano ya kina kama suluhu ya migogoro na kinzani zinazojitokeza katika maisha ya mwanadamu, kwani kushindwa kwa misingi ya amani matokeo ya vita!

Hivi ndivyo Kardinali Leonardo Sandri, Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa kwa ajili ya Makanisa ya Mashariki anavyomkumbuka Mwenyeheri Yohane Paulo wa Pili, kama sehemu ya Katekesi endelevu za Kipindi cha Kwaresima na kama sehemu ya mchakato wa maandalizi ya maadhimisho ya kumtangaza kuwa Mtakatifu. Tafakari hii imetolewa kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Giusto Jimbo Katoliki Trieste, Italia.

Mwenyeheri Yohane Paulo wa Pili alipenda kujikita katika amani kwa njia ya majadiliano ya kidini na kiekumene, mambo ambayo yalikuwa yanabubujika kutoka katika undani wa tasaufi yake; iliyounganisha mawazo na matendo yaliyomwilishwa katika uhalisia wa maisha ya mwanadamu. Kwa njia hii, Mwenyeheri Yohane Paulo II alifanikiwa kuleta mageuzi makubwa duniani na kwa namna ya pekee Barani Ulaya. Kuta za chuki na uhasama wa kisiasa zikamobolewa, wananchi wakapata uhuru wa kujenga na kudumisha mshikamano wa upendo na kidugu.

Mwenyeheri Yohane Paulo wa Pili aliyeonja suluba na mateso ya vita kuu ya pili ya dunia, aliweka dhana ya amani kuwa ni kati ya mafundisho yake makuu, kwa waamini na wale wasioamini, kwani vita inapofumuka haina pazia wala macho! Kwa mwamini, amani ni kielelezo makini cha ufuasi wa Kristo na kwamba, hii ni zawadi ambayo Kristo amewaachia wafuasi wake, hivyo wanayo dhamana ya kulinda, kuitetea na kuiendeleza, kwa kuanzia kwa wao wenyewe ambao wanapaswa kuwa kweli ni vyombo vya amani.

Mwenyeheri Yohane Paulo wa Pili anasema Kardinali Sandri kwamba, hakusita kuwakemea viongozi wa Jumuiya ya Kimataifa waliokuwa wanatumia vita kama njia ya kufikia suluhu na maamuzi yao ya kisiasa. Kardinali Sandri anasema, kamwe hatasahau pale aliposimama kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican kuitangazia dunia kwamba, Papa Yohane Paulo II amefariki dunia. Moyo wake ulishikwa na simanzi na huzuni kubwa sana!








All the contents on this site are copyrighted ©.