2014-04-10 12:15:29

Yohane XXIII na Yohane Paulo II ni miamba wa imani na utakatifu wa maisha!


Kardinali Agostino Vallini, Makamu Askofu Jimbo kuu la Roma katika Barua yake kwa waamini wa Jimbo kuu la Roma anasema kwamba, tukio la Mama Kanisa kuwatangaza Wenyeheri Yohane wa XXIII pamoja na Yohane Paulo II kuwa watakatifu hapo tarehe 27 Aprili 2014 ni tukio la neema na baraka kwa Kanisa zima, linalopokelewa na Jimbo kuu la Roma kwa mikono miwili. Hawa ni miamba wawili walioasisi na kumwilisha Mafundisho ya Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican. RealAudioMP3

Ni Maaskofu waliotekeleza utume na maisha yao hapa Roma kama Makhalifa wa Mtakatifu Petro; wakawa ni waalimu wa imani, maadili na utu wema kwa njia ya ushuhuda wa maisha yao. Ni viongozi waliojitosa kimasomaso kutangaza Habari Njema ya Wokovu hadi miisho ya dunia, wakitoa kipaumbele cha pekee kwa maskini na wote waliokuwa wanasukumizwa pembezoni mwa Jamii kutokana na hali n anafasi zao katika Jamii iliyokuwa inawazunguka.

Viongozi hawa wawili, walikazia kwa namna ya pekee kabisa umuhimu wa adhimisho la Fumbo la Ekaristi Takatifu kama kiini na kilele cha maisha na utume wa Kanisa, kwa kutoa mwaliko kwa waamini kushiriki kikamiluifu katika Ibada ya Misa Takatifu. Hii ilikuwa ni njia muafaka ya kujenga na kudumisha uhusiano kati ya mwamini na Yesu Kristo unaopaswa pia kuendelezwa kwa njia ya sala na maisha adili.

Mwenyeheri Yohane XXIII kwa ushupavu na imani thabiti, alithubutu kufungua ukurasa mpya wa maisha na utume wa Kanisa kwa kuitisha Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican, ambao Kanisa linaendelea kushuhudia matunda yake, kwa kusoma alama za nyakati. Yohane Paulo II katika maisha na utume wake kama Khalifa wa Mtakatifu Petro, alijitahidi kumwilisha Mafundisho ya Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican, changamoto na mwaliko kwa waamini kuendelea kufanya rejea katika Mafundisho ya Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican na hatimaye, kuyamwilisha katika uhalisia wa maisha na vipaumbele vyao.

Kardinali Agostino Vallini anawaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema, kutumia kipindi hiki cha Kwaresima kama sehemu ya mchakato wa maandalizi ya kushiriki kikamilifu katika mchakato wa Mama Kanisa wa kuwatangaza Wenyeheri Yohane wa XXIII na Yohane Paulo II kuwa ni watakatifu, hapo tatehe 27 Aprili 2014, Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro utakapofurika kwa umati mkubwa wa waamini na mahujaji kutoka sehemu mbali mbali za dunia.








All the contents on this site are copyrighted ©.