Ujumbe wa Papa Francisko kwa Siku ya Vijana Kijimbo kwa Mwaka 2014
Jumapili ya Matawi, Kanisa linaadhimisha Siku ya Vijana Duniani katika ngazi ya Kijimbo,
inayoongozwa na kauli mbiu “Heri maskini wa roho, maana ufalme wa mbingu ni wao”.
(Mt. 5:3).
Baba Mtakatifu
Francisko katika ujumbe wake kwa Maadhimisho ya Siku ya 29 ya Vijana Duniani kwa Mwaka
2014, bado anakumbuka maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani iliyofanyika mjini Rio
de Janeiro, Brazil.
Hili lilikuwa ni tukio la imani na udugu, lililopambwa
na kupambika kwa wema pamoja na ukarimu wa wananchi wa Brazil ulioshuhudia umati mkubwa
wa vijana ukifurika katika ufuko wa Copacabana, changamoto kwa kila mwamini kuendelea
kuwa ni mfuasi wa Yesu na Mmissionari, ili kuweza kuwashirikisha wengine hazina hii
muhimu katika maisha.
Siku ya Vijana Duniani kwa Mwaka 2016 itaadhimishwa Jimbo
kuu la Krakovia, nchini Poland. Katika kipindi cha miaka mitatu, vijana wataendelea
kutafakari juu ya Heri za Mlimani. Mwaka huu, vijana wanatafakari kuhusu Heri ya kwanza,
yaani “Heri maskini wa roho, maana ufalme wa mbingu ni wao”. Kwa mwaka 2015 vijana
wanaalikwa kutafakari kuhusu “Heri wenye usafi wa moyo, maana ufalme wa mbingu ni
wao” na kwa Mwaka 2016 kauli mbiu ni “Heri wenye huruma, maana hao watahurumiwa”.
Baba Mtakatifu Francisko anawahamasisha vijana kufanya tafakari ya Heri za
Mlimani kwani haya ni Mafundisho Makuu ya Yesu aliyoyatoa pale kando la Ziwa la Galilaya.
Mlimani kadiri ya Maandiko Matakatifu ni mahali pa ufunuo ambako Mwenyezi Mungu anapenda
kukutana na watu wake. Yesu anatumia fursa hii ili kuwashirikisha wafuasi wake chemchemi
ya maisha, kwa kujifunua kama Mwalimu na Musa mpya.
Yesu anajionesha kuwa
ni njia inayobubujika furaha tangu pale alipozaliwa hadi alipokufa juu ya Msalaba
na hatimaye, kufufuka siku ya tatu, matukio yote haya yanaonesha jinsi ambavyo alimwilisha
Heri za Mlimani katika maisha yake na kukamilisha ahadi za Ufalme wa Mungu. Yesu anawaalika
wafuasi wake kutembea pamoja na ye katika njia ya upendo inayowapeleka katika uzima
wa milele. Hii njia inayosheheni magumu, lakini Yesu ameahidi kwamba, ataendelea kuwa
pamoja nao hadi utimiifu wa dahali. Watakumbana na umaskini, watateswa na kunyanyaswa,
watapamba na na ukosefu wa haki na changamoto za toba ya wongofu wa ndani, bila kusahau
mapambano yanayowataka kuchuchumilia utakatifu wa maisha.
Kwa hakika anasema
Baba Mtakatifu, watakabiliana na changamoto mbali mbali za maisha, mwaliko wa kuendelea
kushirikiana na Yesu katika furaha na mateso, katika magumu na hali ya kukata tamaa.
Kwa kushikamana na Yesu anasema Baba Mtakatifu, waamini wataweza kupata amani na furaha
inayobubujika kutoka kwenye upendo wa Mungu usiokuwa na mipaka. Heri za Mlimani ni
nguvu ya mabadiliko mapya inayoleta mageuzi ya furaha ya kweli na wala si kama ile
inayotolewa na vyombo vya upashanaji habari. Inashangaza masikioni mwetu kwamba, Mwenyezi
Mungu amejitwalia ubinadamu, akawa sawa na binadamu, hata kufa Msalabani.
Kwa
mantiki ya ulimwengu huu, wale ambao wanahesabiwa na Yesu kuwa wana heri, ni watu
wanyonge na waliopoteza dira na mwelekeo! Wanatukuzwa wale wanaoonesha mafanikio,
wenye mamlaka, nguvu na wenye kuheshimiwa na watu! Hii ni changamoto kubwa ya imani,
inayowaalika vijana kuchukua Msalaba wao na kuanza safari ya kumfuasa Yesu, kwani
Yeye anayo maneno ya uzima. Vijana wakithubutu kumkubali na kumpokea Yesu katika maisha
yao ya ujana, atawajaza furaha na maana halisi ya maisha!
Baba Mtakatifu anawahamasisha
vijana kuwa ni watu wenye furaha inayosimikwa katika imani na ukweli, mambo yatakayowawezesha
kuwa na mang’amuzi ya kweli katika maisha kwa kukataa njia za mkato ambazo mara nyingi
zinahatarisha maisha yao kwa kuwatumbukiza katika raha, starehe na anasa, mambo ambayo
kamwe hayawezi kuzima kiu ya maisha yao ya ndani. Inasikitisha kumwona kijana akiogelea
katika utupu!
Vijana wanapaswa kuwa imara wakiwa wanaongozwa na Neno la Mungu
katika maisha yao, tayari kushindana na malimwengu, wakiwa na ujasiri unaowaongoza
kutafuta furaha ya kweli pamoja na kuzingatia mambo msingi katika maisha. Kwa njia
hii vijana wataweza kuwajibika na kukabiliana na changamoto za maisha kwa ujasiri
mkuu.
Baba Mtakatifu anasema, umaskini wa roho unajionesha kwa namna ya pekee
katika Fumbo la Umwilisho, pale Yesu alipojitwalia hali ya binadamu akawa sawa na
binadamu na wala hakuona kwamba, kuwa sawa na Mungu ni jambo la kung’ang’ania sana.
Hapa Mwenyezi Mungu anaamua kuukumbatia umaskini, ili aweze kumtajirisha mwanadamu
kwa umaskini wake. Hili ndilo Fumbo la Umwilisho linalopata utimilifu wake katika
Fumbo la Pasaka, kwa kuonesha unyenyekevu na upendo wa hali ya juu kabisa kwa mwanadamu.
Mtakatifu Francisko wa Assisi ni kielelezo na mfano wa kuigwa katika umaskini wa roho,
kwa kuonesha upendo kwa Kristo, maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii.
Umaskini
wa roho ni changamoto na mwaliko wa kubadilisha mfumo wa maisha kwa kuwa huru na vitu
wala kutokubali kumezwa na malimwengu: utajiri na mali na matokeo yake mambo haya
yanawaachia machungu katika maisha. Vijana wanahamasishwa kujiaminisha mbele ya Mungu
anayewapenda na kamwe hatawasahau, jambo la msingi ni kuwa na ujasiri wa furaha na
kiasi. Vijana wanaalikwa na Mama Kanisa kwa namna ya pekee kutubu na kuongoka, kwa
kukazia upendo na mshikamano wa kidugu katika mchakato wa kukabiliana na hali ya umaskini
unaojionesha katika: ukosefu wa fursa za ajira, wahamiaji, matumizi haram ya dawa
za kulevya na utumwa mamboleo. Vijana wawe ni kikolezo cha: ujasiri, upendo na matumaini
mapya miongoni mwa vijana wenzao. Maskini ni fursa ya kukutana na Yesu mteseka!
Baba
Mtakatifu anasema hata maskini katika umaskini wao, wanayo mengi ya kuwashirikisha
na kuwafundisha. Hawa ni kama Mtakatifu Benedikto Giuseppe Labre aliyekuwa analala
kwenye mitaa ya mji wa Roma, lakini alibahatika kuwa ni mshauri mkuu wa maisha ya
kiroho hata kwa watu mashuhuri kwenye Karne ya kumi na nane. Utu wa mtu una thamani
kubwa na wala si kiasi cha fedha alicho nacho kwenye akaunti yake Benki. Maskini ni
walimu wa unyenyekevu na matumaini kwa Mungu, wanaotambua udhaifu wao, tayari kukimbilia
huruma na upendo wa Mungu.
Baba Mtakatifu anasema, Yes uni kiini cha Habari
Njema ya Wokovu na ujenzi wa Ufalme wa Mungu ambao Mama Kanisa anasali daima ili uweze
kuwafikia watu wengi zaidi, kwa kuhakikisha kwamba, Wakristo wanajitokeza kifua mbele
kwenda kuwatangazia watu Habari Njema ya Wokovu hadi miisho ya dunia. Kanisa halina
budi kukumbatia Ufukara wa Kiinjili ili kuwatangazia maskini Habari Njema ya Wokovu.
Uinjilishaji Mpya unawezekana tu, ikiwa kama utakuwa unabubujika kutoka katika Injili
ya Furaha. Waamini wajenge na kuimarisha uhusiano na Mungu pamoja na jirani zao.
Kutangazwa
kwa Wenyeheri Yohane wa XXIII na Yohane Paulo II kuwa Watakatifu liwe ni tukio linaloshehenesha
furaha ya kweli miongoni mwa wafuasi wa Kristo na watu wote wenye mapenzi mema. Yohane
Paulo II atakuwa ni mtakatifu msimamizi wa Siku za Vijana Duniani, kwani Yeye ni muasisi
na mtekelezaji mkuu wa Maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani. Kwa vijana wengi ataendelea
kuwa ni Baba na Rafiki.
Kanisa pia linafanya kumbu kumbu ya Miaka 30 tangu
Vijana walipokabidhiwa Msalaba wa Ukombozi, ambao umetembelea sehemu mbali mbali za
dunia. Kunako Mwaka 1984, Mwenyeheri Yohane Paulo II aliwataka vijana kuutembeza Msalaba
wa Jubilee kuu ya Mwaka wa Ukombozi, kama kielelezo cha upendo wa Kristo aliyeteswa,
akafa na kufufuka ili kumkomboa mwanadamu kutoka katika lindi la dhambi na mauti.
Baba
Mtakatifu Francisko anahitimisha ujumbe wake kwa Siku ya Vijana Kijimbo kwa kusema
kwamba, utenzi wa Bikira Maria, yaani “Magnificat” ni kielelezo cha mwanamke aliyejitahidi
kumwilisha Heri za Mlimani. Injili ya Furaha inabubujika kutoka katika moyo wa Bikira
Maria, ambaye vizazi vyote watamwita Mwenyeheri. Bikira Maria nyota ya Uinjilishaji
Mpya awasaidie waamini kumwilisha Injili na Heri za Mlimani katika maisha kwa kuwa
na ujasiri wa furaha.
Ujumbe huu umehaririwa na Padre Richard A. Mjigwa,
C.PP.S. Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.