2014-04-10 14:52:36

Onesheni thamani kwa Mji wa Roma, boresheni maisha kwa masomo na tunu bora za maisha ya kiroho!


Baba Mtakatifu Francisko, Alhamisi tarehe 10 Aprili 2014 amekutana na kuzungumza na Jumuiya ya Chuo Kikuu cha Kipapa cha Gregoriani, Taasisi ya Maandiko Matakatifu na Taasisi ya Kanisa la Mashariki. Baba Mtakatifu anasema hizi ni taasisi ambazo ziliunganishwa na Papa Pio kumi na moja kunako mwaka 1928 na kukabidhiwa chini ya usimamizi wa Shirika la Wayesuit, kwa ajili ya kumtumikia Kristo, Kanisa na kuendelea kuwa waaminifu kwa Khalifa wa Mtakatifu Petro.

Baba Mtakatifu anakazia umuhimu wa ushirikiano kwa kuendeleza kumbu kumbu za kihistoria ili kuziendeleza kwa siku za usoni kwa kuzingatia kipaji cha ugunduzi, kinachowawezesha kupata mwelekeo mpana zaidi wa hali na changamoto mamboleo ili kushirikishana na kuzipatia ufumbuzi kwa kutumia njia bora zaidi.

Baba Mtakatifu anaitaka Jumuiya ya Chuo Kikuu cha Kipapa cha Gregoriani na taasisi zake kuhakikisha kwamba, inathamini eneo wanalofanyia kazi na kusomea, yaani Jimbo kuu la Roma. Hapa ni kuna mizizi ya imani, kumbu kumbu hai ya Mitume na Wafiadini; ni mahali panapoonesha ukarimu, umoja na Ukatoliki. Hizi ni tunu zinazopaswa kuheshimiwa na kuthaminiwa na wote.

Roma ni mji ambao unakusanya waamini kutoka katika Makanisa mahalia, wanaokuja wakiwa na tamaduni na mapokeo yao; utajiri mkubwa kwa vyuo vikuu vya kipapa pamoja na taasisi zake, changamoto ya kukuza na kuimarisha imani, kwa kufungua akili na mioyo ili kuona Ukatoliki. Ni mwaliko wa kutoka pembezoni mwa jamii na kuingia mjini kati, tayari kurudi tena pembezoni mwa Jamii kwa ajili ya kuhudumia.

Baba Mtakatifu anasema, kuna haja ya kuhakikisha kwamba, kunakuwepo na uwiano bora zaidi kati ya masomo na maisha ya kiroho, kwa kurutubisha mahusiano haya kwa kuonesha upendo thabiti kwa Yesu Kristo na Kanisa lake; kwa kujikita katika tafiti moyo inayogusa ukweli na imani; mambo yanayofafanuliwa kwa kina na mapana katika masomo ya Falsafa na Taalimungu yanayojikita katika sala, kwa kujinyenyekeza mbele ya Mwenyezi Mungu, ili kutafuta ukweli ili kuuendeleza: kuuimarisha kadiri muda unavyozidi kusonga mbele. Mwanataalimungu asiyesali wala kumwabudu Mwenyezi Mungu anaweza kuishia katika utupu!

Baba Mtakatifu anasema, tafiti na masomo ni mambo ambayo hayana budi kumwilishwa katika maisha ya mtu binafsi na jumuiya; katika dhamana ya kimissionari na udugu unaowashirikisha hata maskini pamoja na kuhangaikia maisha ya ndani ili kujenga na kuimarisha uhusiano na Yesu. Vyuo vikuu na Taasisi za elimu ya juu ni Jumuiya zinazowasaidia wanafunzi kukua na kukomaa kama ilivyo kwenye familia.

Viongozi wa Vyuo vikuu na taasisi za elimu ya juu ni wakuu wa Jumuiya, changamoto ya kuonesha ari na moyo wa huduma ili kujenga na kuimarisha tunu msingi za kifamilia katika uhalisia wa maisha ya kila siku unaojikita katika ubinadamu na hekima, ili kuwajengea wanafunzi wanaohitimu masomo yao, kuweza kutangaza kweli mintarafu ubinadamu. Bila kuthamini wema na uzuri wa familia, kazi itageuka kuwa ni shughuli ya akili isiyokuwa na mashiko; mshika maadili pasi na wema; mtaalam pasi na elimu wala uzuri, mtu anayeendeshwa na taratibu za kila siku.

Baba Mtakatifu Francisko anasema kwamba, mwingiliano wa kila siku unaojikita katika kazi na ushuhuda unaotolewa na wafanyakazi wanaotekeleza dhamana yao kwenye Chuo kikuu na Taasisi mbali mbali, watawaonjesha ukweli utakaosaidia sayansi wanazojifunza kuwa kweli ni sayansi za kiutu na wala si maabara tu ya kuunda wasomi.

Baba Mtakatifu anaitakia kheri na baraka tele Jumuiya ya Chuo Kikuu cha Kipapa cha Gregoriani pamoja na taasisi zake kwa kuwaweka chini ya maombezi ya Bikira Maria kikao cha hekima na ya Mtakatifu Inyasi wa Loyola pamoja na watakatifu somo na wasimamizi wao.







All the contents on this site are copyrighted ©.