Membe: Hakuna maendeleo bila kushirikiana na sekta binafsi
Tanzania itaendelea kufanya jitihada kubwa na kwa hakika itakufa ikijaribu kuimarisha
ushirikiano wa karibu zaidi kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi, kama njia bora
zaidi ya kuleta na kudumisha maendeleo endelevu ya kiuchumi nchini. Aidha, Tanzania
imesisitiza kuwa nchi za Afrika ni lazima ziendelee kutafuta namna ya kumaliza migogoro
na mizozo yake ya kisiasa na kijeshi, kama msingi mkuu wa kutafuta na kupata maendeleo
endelevu na ya kudumu ya kiuchumi kwa watu wake.
Hayo yameelezwa Jumatano,
Aprili 9, 2014 na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bwana Bernard
Membe, wakati alipopokea Tuzo la Kiongozi Mwenye Mchango Mkubwa Zaidi Katika Maendeleo
ya Bara la Afrika kwa mwaka 2013 ambalo ametunikiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete.
Akizungumza katika sherehe ya kutunuku
Tuzo hiyo kwa Mheshimiwa Rais Kikwete kwenye Hoteli ya St. Regis mjini Washington,
D.C., Mheshimiwa Membe amesema kuwa uzoefu wa Tanzania unaonyesha kuwa ushirikiano
na uhusiano wa karibu kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi ni msingi mkuu wa maendeleo
ya nchi yoyote, ikiwamo Tanzania.
Amesema kuwa ushirikiano kati ya sekta hizo
mbili umeleta manufaa na faida kubwa katika maendeleo ya Tanzania katika sekta za
huduma za jamii na katika huduma za kiuchumi. Waziri Membe amesema kuwa mifano ya
mafanikio ya ushirikiano kati ya sekta hizo mbili ni wazi katika sekta kama ya elimu
ambako Tanzania imefanikiwa kufikia Malengo ya Maendeleo ya Milenia katika usajili
wa watoto kuingia shule na katika kuleta usawa katika watoto wa kike na kiume wanaoandikishwa
kuanza shule kwa sababu Sekta Binafsi inasaidiana na Sekta ya Umma katika kuwekeza
katika elimu.
“Kwa sababu ya ushirikiano huo wa karibu, sisi katika Serikali,
tumefanya uamuzi kwamba mikopo ya wanafunzi isitolewe kwa wananchi wanaosoma kwenye
vyuo vya umma pekee bali kwa wanafunzi wote wakiwamo wale wanaosoma katika vyuo vikuu
binafsi. Hivyo, uhusiano kati ya sekta hizo mbili umeleta mafanikio makubwa katika
sekta hiyo ya elimu,” amesema Bwana Membe.
Waziri Membe pia ametaja mafanikio
makubwa yaliyopatikana katika maeneo mengine ya maendeleo kwa sababu ya ushirikiano
huo yakiwemo ya utunzaji wa mazingira, usambazaji wa huduma ya maji safi na salama,
uboreshaji wa huduma za afya, maendeleo ya miundombinu hasa ya barabara na uboreshaji
wa huduma katika kilimo.
Aidha, Waziri Membe amezungumzia hatua zinazochukuliwa
na Serikali kuleta uwazi na usimamizi mzuri katika sekta ya gesi hata kabla ya Tanzania
haijaanza kuchimba gesi akisisitiza kuwa bila uwazi sekta hiyo itagubikwa na utawala
duni, rushwa na usimamizi dhaifu.
Kuhusu umuhimu wa amani kama sharti la Maendeleo
ya Afrika, Waziri Membe amesema kuwa uzoefu wa Afrika na dunia nzima unaonyesha kuwa
hakuna maendeleo yoyote na hasa ya kiuchumi bila kuwepo na amani.
Wakati huo
huo, Waziri Membe amekutana na kufanya mazungumzo na Gavana wa Jimbo la Maryland,
Mheshimiwa Mark O’Malley katika mazungumzo yaliyofanyika kwenye Hoteli ya St. Regis
mjini Washington, Marekani. Katika mazungumzo hayo, Mheshimiwa Membe amemwalika Gavana
O’Malley kutembelea Tanzania na kutumia nafasi yake kuhakikisha kuwa Jimbo la Maryland
linaanzisha ushirikiano na mkoa mmojawapo wa Tanzania.