Kanisa linaomboleza kifo cha Askofu mkuu Boniface Lele
Askofu mkuu mstaafu Boniface Lele wa Jimbo kuu la Mombasa, Kenya amefariki dunia akiwa
na umri wa miaka sitini na sita kutokana na ugonjwa wa shinikizo la damu. Askofu mkuu
mstaafu Lele, Ijumaa tarehe 4 Aprili 2014 alilazwa Hospitalini Mombasa, akiwa na hali
mbaya na tarehe 10 Aprili 2014 akafariki dunia kutokana na ugonjwa wa shinikizo la
damu.
Kardinali John Njue, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Kenya anasema,
kifo cha Askofu mkuu mstaafu Boniface Lele wa Jimbo kuu la Mombasa ni pigo kubwa sana
kwa Kanisa. Ni kiongozi aliyejitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya ustawi na maendeleo
ya Kanisa Jimbo Katoliki la Kitui na baadaye, Jimbo kuu la Mombasa. Ni kiongozi aliyekuwa
mpole na mnyekevu, kweli atakumbukwa na wengi.
Kardinali Njue anawaalika waamini
kumsindikiza Marehemu Askofu mkuu mstaafu Lele kwa sala na sadaka zao, ili aweze kupata
pumziko la milele, miongoni mwa watakatifu wa Mungu. Familia ya Mungu Jimbo kuu la
Mombasa, baada ya kupata taarifa hii ilikusanyika na kusali kwenye Hospitali ya Pandya,
mahali ambako mwili wa Marehemu Askofu mkuu mstaafu Lele unahifadhiwa.