2014-04-09 15:22:54

Patriaki mstaafu Emmanuel III Delly amefariki dunia


Baba Mtakatifu Francisko amepokea kwa majonzi makubwa habari za kifo cha Patriaki Mstaafu Emmanuel Delly wa tatu wa Kanisa la Babiloni ya Wakaldea, kilichotokea Jumatano tarehe 9 Aprili 2014, huko San Diego, Calfonia, nchini Marekani. Amefariki dunia akiwa na umri wa miaka 87 na Ibada ya mazishi inafanyika Jumamosi, tarehe 12 Aprili 2014 huko Detroit, Marekani.

Katika salam zake za rambi rambi kwa Patriaki Louis Raphael Sako wa kwanza, Baba Mtakatifu anapenda kuwahakikishia wote walioguswa na msiba huu, uwepo wake wa karibu kwa waamini wote wanaoishi ndani na nje ya Iraq. Marehemu Patriaki mstaafu alikuwa ni kiongozi aliyejitoa kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya watu wake; akahimiza watu kuheshimiana na kutendeana kwa haki na amani sanjari na kukuza majadiliano ya kidini na waamini wa dini mbali mbali.

Baba Mtakatifu anasema, anaungana na wote wanaoomboleza msiba wa Patriaki mstaafu Emmanuel Delly wa tatu na kwamba, anaiombea roho ya marehemu ipate kuonja huruma na upendo wa Mwenyezi Mungu, ili iweze kupumzika kwa amani.

Kardinali Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican naye pia ametuma salam zake za rambi rambi kutokana na msiba huu mzito uliolikumba Kanisa. Historia ya maisha yake inaonesha kwamba, Marehemu Patriaki Emmanuel Delly wa tatu alizaliwa tarehe 27 Septemba 1927. Baada ya masomo na majiundo yake ya Kikasisi, akapewa Daraja Takatifu la Upadre tarehe 21 Desemba 1952. Tarehe 19 Aprili 1963 akawekwa wakfu kuwa Askofu na kushiriki katika Maadhimisho ya Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican.

Tarehe 6 Mei 1967 akateuliwa kuwa ni Askofu mkuu wa jimbo kuu la Kaskar na msaidizi wa Patriaki wa Babiloni ya Wakaldei hadi tarehe 24 Oktoba 2002, alipong'atuka kutoka madarakani kutokana na umri.







All the contents on this site are copyrighted ©.