2014-04-09 14:36:10

Msalaba kutoka Lampedusa kutembezwa nchini Italia


Kisiwa cha Lampedusa, kilicho Kusini mwa Italia kimekuwa maarufu sana sehemu mbali mbali za dunia kutokana na ukweli kwamba, hapa ndipo kituo kikuu cha matumaini ya wakimbizi na wahamiaji kutoka Afrika wanaotafuta nafuu na maboresho ya maisha yao Barani Ulaya, lakini kwa bahati mbaya, wengi wao wanafariki dunia hata kabla ya kufika Ulaya!

Wananchi wa Lampedusa wametengeneza Msalaba ambao umebarikiwa na Baba Mtakatifu Francisko wakati wa Katekesi yake Siku ya Jumatano, tarehe 9 Aprili 2014 kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican. Msalaba huu ni mabaki ya mitumbwi na mashua zilizozama majini au kutelekezwa kwenye ufuko wa bahari, Kusini mwa Italia. Msalaba utatembezwa nchini Italia, ili kusambaza ujumbe wa mshikamano na amani kati ya Jumuiya, Parokia, Tamaduni, Miji na watu wa imani mbali mbali.

Msalaba huu baada ya kutembezwa kwenye Parokia mbali mbali nchini Italia hatimaye, utatunzwa kwenye Kanisa la Mtakatifu Stefano, Jimbo kuu la Milano, Italia. Msalaba huu ni changamoto ya mshikamano wa sala na mapendo kwa wakimbizi na wahamiaji wanaopoteza maisha yao kwa kufa maji baharini, hata kabla ya kufika kwenye "Nchi za ahadi, zilizojaa asali na maziwa"







All the contents on this site are copyrighted ©.