2014-04-09 09:24:24

Kanuni msingi katika kudumisha majadiliano ya kidini


Kardinali Jean Louis Tauran, Rais wa Baraza la Kipapa la majadiliano ya kidini hivi karibuni alifanya ziara ya kichungaji nchini Benin, iliyoongozwa na kanuni zifuatazo: kujionea mwenyewe, kusikiliza kwa makini, kuelewa na kuwatia moyo wadau mbali mbali katika mchakato wa majadiliano ya kidini. RealAudioMP3

Akiwa nchini Benin, Kardinali Tauran alifanikiwa kukutana na kuzungumza na viongozi wa Kanisa, Serikali na waamini wa dini mbali mbali walioonesha utashi wa kujenga na kudumisha misingi ya majadiliano ya kidini kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya wananchi wa Benin na Afrika katika ujumla wake.

Baraza la Maaskofu Katoliki Benin limefafanua mipango na mikakati yake ya kichungaji katika mchakato wa majadiliano ya kidini pamoja na harakati zinazofanywa na Kanisa katika kuwatangazia watu Injili ya Furaha kama anavyosisitizia Baba Mtakatifu Francisko. Serikali ya Benin imefafanua mikakati inayotekelezwa katika kukuza na kudumisha amani na utulivu nchini humo kwa kuwahusisha wananchi wote wa Benin.

Kardinali Tauran amesikiliza maoni, changamoto na ugumu wanaokabiliana nao katika utekelezaji wa mikakati hii katika uhalisia wa maisha. Jumuiya ya Seminari kuu ya Benin imeelezea jinsi ambavyo hata katika dini asilia za Kiafrika, waamini hao wanaweza kuona kile kilicho kweli na kitakatifu kama ambavyo Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican wanavyokazia katika Waraka wake kuhusu majadiliano ya kidini na waamini wa dini mbali mbali duniani. Jumuiya hii imeonesha jinsi ambavyo Kanisa nchini Benin linavyokabiliana na changamoto mbali mbali katika mchakato wa utamadunisho wa tunu msingi za Kiinjili Barani Afrika.

Kardinali Tauran amepata fursa ya kujionea kwa macho yake mwenyewe amani na utulivu miongoni mwa wananchi wa Benin, kama nyenzo msingi ya maendeleo na ustawi wa wengi. Katika makala yaliyoandikwa kwenye Hazeti la L’Osservatore Romano na Padre Chidi Denis Isizoh, Afisa kutoka Baraza la Kipapa la Majadiliano ya Kidini anasema kwamba, kuna maneno makuu manne yanayopaswa kuwa ni msingi wa majadiliano ya kidini miongoni mwa waamini wa dini mbali mbali. Maneno haya ni: kuheshimiana, kufahamiana, kupendana na kuelewana. Maneno haya yakimwilishwa katika uhalisia wa maisha, amani na utulivu vinaweza kudumishwa miongoni mwa watu wa mataifa.

Kardinali Tauran alipata fursa pia ya kutembelea Mlango wa Ukombozi na Kanisa kuu la Bikira Maria Mkingiwa Dhambi ya Asili. Hapa ni mahali ambapo Wamissionari wa kwanza waliojitosa kimasomaso kutangaza Habari Njema ya Wokovu wanapumzika katika usingizi wa amani. Akiwa katika eneo hili, Kardinali Tauran ametembelea pia kaburi la Hayati Kardinali Bernardin Gantin, Mwafrika wa kwanza kupewa dhamana ya kuongoza Baraza la Kipapa la haki na amani na hatimaye, kuwa ni Dekano wa Makardinali.

Kardinali Tauran akiwa Seminari kuu ya Mtakatifu Gallo mjini Ouidah, alipata nafasi ya kuzungumza na Majandokasisi wanaojiandaa kwa maisha na wito wa Kipadre ndani na Nje ya Benin. Amekazia umuhimu wa majiundo makini: kiroho, kimwili, kiakili, kiutu na kichungaji, yatakayowasaidia kutekeleza dhamana na wajibu wao kwa moyo mkuu katika kipindi hiki cha Uinjilishaji Mpya, ambacho kinadai ushuhuda wa maisha adili na utakatifu wa maisha.

Kardinali Tauran amewashukuru wadau mbali mbali wanaoendelea kujielekeza katika mchakato wa Majadiliano ya Kidini, ili kujenga na kudumisha misingi ya haki, amani, upendo, udugu na mshikamano wa kitaifa. Kanisa litaendeleza majadiliano ya kidini na waamini wa dini mbali mbali duniani kama sehemu ya utekelezaji wa Mafundisho ya Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican sanjari na mchakato wa utamadunisho wa tunu msingi za Kiinjili Barani Afrika.








All the contents on this site are copyrighted ©.