Papa Yohane XXIII na Papa Yohane II mchango wao kwa Kanisa Barani Afrika
Kanisa Barani Afrika tangu Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican hadi mapambazuko ya Millenia
ya tatu ya Ukristo. Mchango wa Papa Yohane XXIII na Papa Yohane II kwa Kanisa Barani
Afrika. Hii ndiyo kauli mbiu itakayofanyiwa kazi na viongozi waandamizi kutoka Vatican
na Familia ya Mungu Barani Afrika, ili kwa pamoja kuweza kuangalia mchango wa wenyeheri
hawa wanaotarajiwa kutangazwa na Mama Kanisa kuwa Watakatifu, hapo tarehe 27 Aprili
2014. Kongamano la siku mbili, litafanyika kwenye Chuo Kikuu cha Kipapa cha Urbainiana
kuanzia tarehe 24 hadi tarehe 25 Aprili 2014.
Miaka hamsini tangu maadhimisho
ya Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican, limekuwa ni tukio la neema na baraka kwa Kanisa
Barani Afrika, katika maisha na utume wake. Familia ya Mungu Barani Afrika imepata
utambulisho wake kitamaduni, kiimani na kijamii, mchango mkubwa uliotolewa na Shirikisho
la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Afrika na Madagascar, SECAM. Tangu baada ya Mtaguso
mkuu wa Pili wa Vatican kumekuwepo na maendeleo makubwa katika maisha na utume wa
Kanisa Barani Afrika. Kongamano hili la siku mbili, litaweza kubainisha mchango wa
Mapapa hawa kwa Kanisa Barani Afrika.