2014-04-08 10:19:52

Ombeeni amani ya Tanzania


Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania, Jumapili iliyopita, tarehe 6 Aprili 2014, limekutana na kusali pamoja na watanzania wanaoishi mjini Roma pamoja na viunga vyake. Mara baada ya Misa Takatifu, Maaskofu, watanzania pamoja na marafiki wa Tanzania walikaa "mkao wa kula" ili kubadilishana mawazo. RealAudioMP3

Askofu mkuu Josephat Lebulu wa Jimbo kuu la Arusha Tanzania, amewataka watanzania wanaoishi na kusoma mjini Roma kujenga na kudumisha msingi wa umoja na udugu kwa kusaidiana na kuimarishana kiimani, ili wakisha imarika wao, waweze pia kuwaimarisha Maaskofu na waamini wengine nchini Tanzania. Amewataka kuzingatia malengo yaliyowaleta Ughaibuni na mara wanapomaliza mkataba wao basi, warejee nchini Tanzania ili kushiriki katika ujenzi wa Ufalme wa Mungu.

Askofu Tarcisius Ngalalekumtwa, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania amewashukuru watanzani kwa kuhudhuria Ibada ya Misa Takatifu, Jumapili ya tano ya Kipindi cha Kwaresima iliyowashirikisha matendo makuu ya Mungu katika kutoa, kulinda na kutetea zawadi ya uhai. Anasema, kuna michakato mbali mbali inayoendelea nchini Tanzania, lakini kwa sasa mchakato mkubwa unaogusa akili na miyo ya watu ni ule wa Katiba Mpya.

Askofu Ngalalekumtwa amewataka watanzania kuombea amani, kwani hali si shwari sana mjini Dodoma, ili Katiba itakayopatikana iwe ni kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya watanzania wote. Amewatakia watanzania wote maandalizi mema kwa ajili ya Maadhimisho ya Fumbo la Pasaka ya Kristo na Pasaka ya kila mwamini.

Kwa upande wake, Askofu mkuu Protase Rugambwa, Katibu mwambata na Rais wa Mashirika ya Kimissionari ya Kipapa, amewataka watanzania wanaoishi na kusoma mjini Roma kuendeleza umoja na mshikamano wa kidugu, kwani umoja miongoni mwa watanzania ni sehemu ya vinasaba vyao. watu wengi wanatamani na kuumeza mate umoja na mshikamano wa watanzania. Amewashukuru na kuwapongeza Maaskofu Katoliki kutoka Tanzania kwa kukubali mwaliko na kushiriki na watanzania wenzao walioko Ughaibuni, Ibada ya Misa Takatifu sanjari na mkao wa pamoja







All the contents on this site are copyrighted ©.