2014-04-08 11:32:12

Msalaba ni kielelezo cha Fumbo la huruma na upendo wa Mungu


Baba Mtakatifu Francisko katika mahubiri yake Jumanne, tarehe 8 Aprili 2014 kwenye Kikanisa cha Mtakatifu Martha, kilichoko mjini Vatican anasema, hakuna Ukristo pasi na Msalaba na kwamba, hakuna mtu anayeweza kujikomboa mwenyewe kutoka katika utumwa wa dhambi na mauti. Msalaba ni kielelezo cha Fumbo la upendo na huruma ya Mungu na wala si pambo Kanisani.

Waisraeli walimlalamikia Mungu katika safari yao kuelekea kwenye Nchi ya ahadi, na huko Jangwani wakaoneshwa che mtema kuni, wakaumwa na nyoka, kielelezo cha uwepo wa dhambi katika maisha ya mwanadamu. Ni nyoka huyu huyu aliyeleta kizaazaa kule kwenye Bustani ya Heden, alipopandisha dhambi na kuonekana kuwa ni kielelezo cha ushindi, lakini akashushwa na kulaaniwa kiasi cha kutembelea tumbo!

Baba Mtakatifu anasema, Yesu alipoinuliwa pale juu Msalabani, ameonesha ushindi dhidi ya dhambi na kifo; akaonesha kwamba, Kristo ni mwana wa mtu, Masiha na mkombozi wa mwanadamu, dira na mwelekeo wa maisha ya Kikristo yanayofumbatwa katika Fumbo la Msalaba. Yesu aliyenyanyuliwa juu ya Msalaba, ni nafsi ya Pili ya Fumbo la Utatu Mtakatifu. Ni Mungu kweli na mtu kweli; aliyejinyenyekesha hata mauti ya Msalaba, ili kumkomboa mwanadamu kutoka katika lindi la dhambi na mauti na hatimaye, kumwonjesha huruma na upendo wa Mungu usiokuwa na kifani.







All the contents on this site are copyrighted ©.