2014-04-08 14:41:27

Maandalizi ya mkutano mkuu wa AMECEA yanazidi kupamba moto


Wajumbe wa Bodi ya Kamati Tendaji ya Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Afrika Mashariki na Kati, AMECEA katika kikao chake kilichofanyika hivi karibuni, mjini Lilongwe, Malawi, kuanzia tarehe 10 – 13 Machi 2014, wameridhika na maandalizi yanayofanywa na Baraza la Maaskofu Katoliki Malawi kwa ajili ya Maadhimisho ya Mkutano mkuu wa AMECEA utakaofanyika mjini Lilongwe, Malawi kuanzia tarehe 16 – 26 Julai 2014.

Waamini na watu wenye mapenzi mema nchini Malawi wanaendelea kuonesha ukarimu wao kwa kuchangia kwa hali na mali katika mchakato unaolenga kufanikisha mkutano mkuu wa AMECEA. Wanaendelea kusubiri kwa hamu na shauku kubwa ili waweze kushiriki katika tukio hili la kihistoria linaliwakusanya Maaskofu na wajumbe mbali mbali kutoka katika nchi wanachama wa AMECEA.

Baraza la Maaskofu Katoliki Malawi linaendelea kushirikiana kwa karibu zaidi na Serikali ya Malawi, ili kuhakikisha kwamba, tukio hili linakuwa ni kwa ajili ya mafao na ustawi wa wananchi wengi wa Malawi. Waamini wanaendelea kusali kwa ajili ya kumwomba Roho Mtakatifu aweze kufanikisha tukio hili. Sala ya kuombea mkutano mkuu wa AMECEA itatumwa kwenye Mabaraza ya Maaskofu Katoliki AMECEA ili iweze kutawanywa Majimboni, Parokiani na Vigangoni, ili kutoa nafasi ya waamini pia kushiriki kikamilifu katika tukio hili la maisha ya kiroho.

Padre Ferdinand Lugonzo, Katibu mkuu wa AMECEA anasema, Sekretarieti ya AMECEA inaendelea pia kukusanya mchango kutoka kwa nchi wanachama na wadau mbali mbali kwa lengo hili. Kwa upande wake, Askofu mkuu Tarcisio Zizaye, Mwenyekiti wa AMECEA amewashukuru Makatibu wakuu kutoka katika nchi za AMECEA katika utekelezaji wa majukumu yao. Amewataka kuhakikisha kwamba, wanafanikisha mkutano huu ambao ni kielelezo cha ushirikiano, mshikamano, umoja na udugu miongoni mwa Maaskofu wa AMECEA.








All the contents on this site are copyrighted ©.