2014-04-08 08:47:16

Kanisa linapania kushiriki kikamilifu katika kudumisha amani na majadiliano ya kidini huko Mashariki ya Kati!


Baba Mtakatifu Francisko, Jumatatu jioni tarehe 7 Aprili 2014 amekutana na kuzungumza na Mfalme Abdullah wa Pili wa Yordan pamoja na ujumbe wake, ambao walipokelewa na Kardinali Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican, aliyekuwa ameandamana na viongozi kadhaa kutoka Vatican.

Baba Mtakatifu na mgeni wake wamefanya mazungumzo yao kwenye Hostel ya Mtakatifu Martha, iliyoko mjini Vatican. Mazungumzo haya kadiri ya taarifa ya Padre Lombardi yamefanyika wakati viongozi hawa wawili wakiwa wanaendelea kupata chai ya jioni na kwamba, yamedumu kwa takribani dakika arobaini na tano.

Safari ya kikazi iliyofanywa na Mfalme Abdallah wa pili mjini Vatican ni sehemu ya maandalizi ya hija ya kichungaji ya Baba Mtakatifu Francisko huko katika Nchi Takatifu, ambako atapata fursa kwanza kabisa ya kutembelea na kuzungumza na wananchi wa Yordan na kwamba, wananchi wengi wa Yordan wanasubiri kwa hamu hija hii ya kichungaji, itakayomwezesha Baba Mtakatifu kujionea hali halisi ya wananchi wa Yordan.

Kwa upande wake, Baba Mtakatifu ameonesha utashi na nia ya kimaadili ya kutaka kushiriki kikamilifu katika mchakato unaopania kupata amani ya kudumu huko Mashariki ya kati pamoja na kudumisha majadiliano ya kidini, kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya wengi. Mwishoni, Baba Mtakatifu amesalimiana na wajumbe waliokuwa kwenye msafara wa Mfalme Abdallah wa pili wa Yordan.







All the contents on this site are copyrighted ©.