Toba, msamaha na upatanisho ni mambo yanayohitaji kifua kipana!
Mpendwa Msikilizaji wa Radio Vatican, Tumsifu Yesu Kristo! Kwa siku hizi arobaini,
pamoja na Mama Kanisa, tupo jangwani, tunasali, tunafunga, tunatoa sadaka na tunashughulikia
kwa uzito zaidi wongofu wa mwenendo wetu.
Tunakiri udhaifu
wetu mbele ya Mungu na mbele za wanadamu wenzetu; tunaomba huruma ya Mungu na msaada
wa sala za ndugu zetu, zitusaidie kuinuka na kuendelea mbele katika safari yetu ya
kumjua Mungu, kumpenda na mwisho kufika kwake.
Mpendwa msikilizaji, baada
ya kuona kwa uchache juu ya hali yetu ya dhambi, leo tuangazie juu ya tunu ya toba,
msamaha na kujirekebisha. Kama ambavyo tunakiri mapungufu yetu na kuomba huruma ya
Mungu atusamehe, papo hapo, kwa mwangwi wa ile sala ya aliyotufundisha Bwana, sisi
nasi tunaomba neema ya kuwasamehe waliotukosea (mt. 6:12), na pia tunaomba neema ya
kuupokea msamaha na kurekebisha makosa yetu.
Tunapotubu kwa moyo kabisa kadiri
ya taratibu za Kanisa, Mungu mwenye huruma anatusamehe makosa yetu. Tunapoomba radhi
kwa wenzetu, nao pia wakitusamehe, ni huruma ileile ya Mungu inakuja kwetu kwa njia
ya zawadi ya msamaha tunaoupokea kutoka kwa wenzetu. Kwa mwangwi huo, tujihekimishe
neno hili, kusamehe ni kuwa chombo cha huruma ya mungu. Mungu anapendezwa na mwanadamu
aliye tayari kusamehe. Mungu anatukuzwa katika kutusamehe sisi makosa yetu (tukitubu
kwa moyo) na anatukuzwa pia katika kusameheana kwetu.
Mpendwa msikilizaji,
katika Jumatano ya majivu neno la Mungu lilitualika sote kufanya TOBA. Kwa leo tuitazame
toba kwa namna mbili. Kwanza toba kama tendo la kawaida kabisa la mwanadamu na pili,
toba kama Sakramenti kadiri ya mafundisho-imani ya Kanisa letu. Katika hilo la kwanza,
kwa kufuata fundisho la Bwana (Mt. 18:22) tunataka kusema, mtu ukimkosea mwenzako,
uwe muungwana tu, jipe moyo; nenda kamwombe msamaha. Usikomae na kujisahaulisha kosa
lako. Kuomba radhi ni tendo la kiutu na ni ujasiri pia. Kuzungumza na kuomba msamaha
kunatupatia nguvu ya kujenga mahusiano mema.
Na sehemu ya pili tunaitazama
toba kama Sakramenti. Tukitenda dhambi, tunatubu/tunaungama kwa moyo wa unyoofu wote.
Sakramenti ya Kitubio ni sakramenti ya Upatanisho. Tunajipatanisha na nafsi zetu,
na binadamu wenzetu na zaidi kabisa tunajipatanisha na Mungu. Sakramenti ya kitubio
ni safari ya maamuzi, mapokezi na sherehe ya Mwana mpotevu anayerudi nyumbani kwa
baba.
Na huko nyumbani kwa baba, huyu mwenye kutubu, anavikwa vazi la neema
aliyoipoteza kwa dhambi, anavikwa viatu kuonesha kuwa amekuwa huru akilini, mwilini
na rohoni, mwana huru wa Mungu, na anavikwa pete kuonesha muungano wake na familia
ya Baba mwema. Kwa mwangwi wa uelewa huo, tunafundishwa juu ya uzito na mafaa ya
sakramenti ya Kitubio, sakramenti ya Utakaso na Upatanisho. Tuipende na tuikimbilie
daima kwani ndipo tunapoguswa nafsi zetu kwa huruma ya Mungu, ndipo tunaporudishiwa
hadhi kwa neema ya utakaso.
Wengi wetu ni majasiri kutenda dhambi, lakini ni
waoga sana kutubu. Matokeo yake tunadhoofika akilini, mwilini na rohoni. Mzaburi anasema
‘nilipoficha dhambi, mifupa yangu ilidhoofika na nyama yangu ikaungulia kama kwenye
joto la Kaskazi...’. Dhambi hudhuru mwili na roho pia. Katika kipindi hiki cha kwaresma
tunaposhughulikia wongofu wetu, tunataka kwa roho ya uwazi na ukweli tujipime na tujiwekee
mkakati kama mwana mpotevu – jasiri tuseme, nitaondoko, nitakwenda kwa baba yangu
na kumwambia...!
Kama Baba Mtakatifu Francisko anavyotuhimiza daima, Mungu
mwenye huruma anatusubiri turudi kwake, yupo tayari kutusamehe, yeye kamwe hachoki
kutusamehe, ni sisi ndiyo tunachoka na tunaona aibu kurudi kwake.Ewe ndugu mpendwa,
tutaishi katika dhambi MPAKA LINI? Amua sasa kwani wakati uliokubaliwa ndio sasa,
wakati wa wokovu ndio huu... (2 Kor 6 : 2 ).
Kama ambavyo sisi tungependa kusamehewa
na Mungu, ni sharti kwanza tuwe tayari kuwasamehe wale waliotukosea. Katika sala ya
Bwana tunasali ‘utusamehe makosa yetu, kama sisi tunavyowasamehe waliotukosea’. Mara
nyingi tunaomba huruma ya Mungu wakati sisi HATUTAKI KABISA, kuwasamehe waliotukosea
hata kama wanatuomba msamaha. Kwa baadhi yetu, kwa nini kusamehe ni kugumu?? Ili tuweze
kusamehe, lazima kwanza tuombe nguvu ya Mungu. Mungu mwenye kutuumbia mioyo safi atusaidie.
Na pili lazima kuamua kusamehe.
Wakati mwingine tunafanya TENDO LA MSAMAHA
bila KUAMUA kusamehe na bila nguvu ya Mungu. Matokeo yake, tutafanya vikao vingi vya
kupatanishana na tutapeana zawadi na kadi nyingi za samahani, lakini vinyongo vinabaki,
kumbukumbu mbaya ya maumivu, hasira na chuki inarudi mara nyingi! Hiyo ni kwa sababu
HUKUAMUA KUSAMEHE, Ulitamka tu maneno ya kusamehe. Wengine tunahalalisha kutokusamehe
kwetu kutokana na uzito wa makwazo tuliyotendewa! Ndugu yangu, hata kama umekosewa
vipi, Msamaha unawezekana, KUSAMEHE INAWEZEKANA. Tuone mifano michache kutoka katika
maandiko matakatifu ya watu waliokanyagwa haswa, lakini WALISAMEHE.
ESAU ANAMSAMEHE
YAKOBO Esau akaja mbio kumlaki Yakobo, akamkumbatia na kumwangukia shingoni akambusu,
nao wakali sana. Mwa. 33:4 . YOSEFU A NAWASAMEHE NDUGU ZAKE! ‘... akasema Basi sasa
msihuzunike wala kufadhaika kwa kuniuza. Mungu ndiye aliyenileta huku niwatangulie
ili niyaokoe maisha ya watu. Akiwa bado analia, Yosefu aliwakumbatia ndugu zake na
kuwabusu. Hapo ndipo ndugu zake walipoweza kuzungumza naye. Mwa. 45: 5, 15. Yosefu
anatufundisha kuona mpango wa Mungu hata katika mambo mabaya.
BABA MWEMA ANAMSAMEHE
MWANA MPOTEVU. Alipokuwa bado yu mbali, baba yake alimwona, na kwa moyo wa huruma
alimkumbatia na kumbusu. Lk. 15: 20b. Hata YESU ALIWASAMEHE WATESI WAKE, Lk. 23:34.
Yesu akasema ‘Baba, uwasamehe kwani hawajui watendalo’. Maandiko matakatifu pia yatuelekeza
kusamehe. Tena iweni wafadhili ninyi kwa ninyi, tena wenye huruma, mkasameheane. [Ef.
4:32]. Vumilianeni na kusameheana iwapo mmoja wenu ana jambo lolote dhidi ya mwenzake.
Mnapaswa kusameheana kama Bwana alivyowasamehe ninyi [Kol. 3:13].
Ndugu yangu
akinikosa, nimsamehe mara ngapi? Hata mara saba? Yesu akamwambia, sikuambii hata
mara saba, bali hata saba mara sabini. [Mt. 18:22]. Na tukisha kusamehewa, tuwe tayari
kurekebisha makosa yetu. Haileti maana kutubu huku unaendelea kutenda kosa lilelile
tena kwa ushupavu zaidi. Kufanya toba ni kuwa tayari kufanya mabadiliko.
Uradhi
wetu na nguvu ya Mungu vitusaidie. Kurekebika ni kuheshimu huruma ya Mungu, kusahihisha
makosa yetu ni kuwaheshimu wale waliotusamehe. Mungu atujalie ujasiri wa kweli, tufanye
toba ya kweli, na tuziache njia zitupelekazo upotevuni.
Kutoka Studio za Radio
Vatican, ni mimi Padre Pambo Martin Mkorwe OSB.