2014-04-07 07:49:38

Tanzania kuna mpasuko!


Askofu Severine Niwemugizi wa Jimbo la Rulenge-Ngara ambaye pia ni Makamu wa Rais, Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania katika mahojiano maalum na Radio Vatican wakati wa hija yao ya kitume mjini Vatican kuanzia tarehe 4 hadi tarehe 8 Aprili 2014 anasema kwamba, Tanzania katika kipindi cha miaka 50 imepita katika hatua kuu mbili; Tanzania iliyokuwa imejengeka katika mshikamano na umoja wa kitaifa kwa kuzingatia mawaidha na ushauri wa wasisi wa taifa la Tanzania. RealAudioMP3

Awamu ya pili ya Tanzania inajionesha kwa namna ya pekee mara baada ya kuingia kwa vyama vingi vya kisiasa, hali ambayo inaonesha mpasuko na misigano kati ya watanzania.

Askofu Niwemugizi anasema, changamoto ni sehemu ya hija ya maisha ya mwanadamu na kamwe haziwezi kukosekana mahali popote pale. Watanzania licha ya umaskini wao, kwa miaka mingi waliendelea kushikamana kama ndugu na kukabiliana na changamoto katika medani mbali mbali za maisha katika umoja, mshikamano na upendo; kweli watanzania walijisikia kuwa ni wamoja, kiasi hata cha kuwajengea majirani zao “wivu mtakatifu”, kwa kuwaona jinsi walivyokuwa wanaishi kwa amani na utulivu! Tanzania ikaonekana kuwa kama ni “Kisiwa na Amani”.

Uwepo wa vyama vingi vya Kisiasa nchini Tanzania, zilikuwa ni dalili za kukomaa kwa siasa na demokrasia kati ya watanzania, lakini ni mchakato uliobeba changamoto nyingi katika maisha ya watanzania wengi. Umoja, upendo na mshikamano wa kitaifa miongoni mwa watanzania ukaanza kuchechemea na watanzania wakaanza kubaguana kwa kufuata itikadi za vyama vyao vya kisiasa, dini na mahali anapotoka mtu. Mivutano na utengano miongoni mwa watanzania vikaanza kushika kasi ya ajabu! Hii inatokana na ukweli kwamba, bado hakuna ukomavu wa kutosha katika vyama vya kisiasa, kwa ajili ya kutafuta mafao ya wengi, umoja, ustawi na maendeleo ya watanzania wote.

Askofu Niwemugizi anasema mchakato wa Katiba Mpya ya Tanzania uliwaonjesha watanzania matumaini mapya kwa kuwa na Katiba Mpya, ambayo kimsingi ni sheria mama. Hapa mpasuko na mgawanyiko wa watanzania: kisiasa na kidini vikajionesha kwa namna ya ajabu kabisa, kila upande unajitahidi kuvutia kwake, umoja wa kitaifa inaonekana kana kwamba, unawekwa rehani!

Askofu Niwemugizi ambaye pia ni Makamu wa Rais, Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania anakiri kwamba, hata ndani ya Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania sauti ya kinabii iliyokuwa na nguvu wakati fulani, imeanza kufifia kutokana na woga wa kupachikwa misimamo ya kisiasa hata kama kimsingi Kanisa halina Chama cha Kisiasa. Askofu Niwemugizi anasema, kuna haja kwa watanzania kuanza tena kwa kasi na ari mpya mchakato wa kujenga na kuimarisha umoja na mshikamano wa kitaifa, kwa kutafuta na kusimamia haki msingi za binadamu, mafao ya wengi na ustawi wa watanzania wote!

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.