Benki ya Vatican kuendelea kutoa huduma kwa Kanisa Katoliki Ulimwenguni
Baba Mtakatifu Francisko amepitisha mapendekezo ya Benko ya Vatican, IOR, kwa siku
za usoni kwa kutambua utume na dhamana yake kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Kanisa
na Vatican katika ujumla wake. Mapendekezo haya yametolewa na tume na kamati mbali
mbali zinazohusika na masuala ya fedha na uchumi mjini Vatican na kuwasilishwa kwa
Baba Mtakatifu na Kardinali Santos Abril Y Castellò, Rais wa Tume ya Makardinali wa
Benki ya Vatican, kama ilivyojadiliwa mwezi Februari 2014.
IOR itaendelea
kutekeleza dhamana na wajibu wake kwa kutoa huduma za Kifedha kwa Kanisa Katoliki
sanjari na kumsaidia Khalifa wa Mtakatifu Petro kutekeleza utume wake kama Kiongozi
mkuu wa Kanisa Katoliki, taasisi pamoja na watu binafsi wanaomsaidia Papa katika utekelezaji
wa majukumu yake. Viongozi wakuu wa Benki ya Vatican wamepewa kazi ya kuhakikisha
kwamba wanawasilisha mipango yao kwa Baba Mtakatifu, Baraza la Makardinali na Baraza
la Kipapa la Uchumi.
Baba Mtakatifu pamoja na mambo mengine, anakazia umuhimu
wa kuzingatia maadili ya kazi, ukweli na uwazi; kanuni na sheria zinazodhibiti masuala
ya fedha mjini Vatican.