Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Mrisho Kikwete amemtumia salamu za
rambirambi Askofu Msaidizi Methodius Kilaini wa Jimbo Katoliki Bukoba, akimpa pole
kwa kifo cha baba yake mzazi, Mzee Paulo Mutegeki Kilaini. Katika salamu hizo zilizotumwa,
Ijumaa, Aprili 4, 2014, Rais Kikwete amemwambia Askofu Kilaini: “Kwa masikitiko makubwa,
nakupa pole nyingi na naungana nawe katika kuomboleza kifo cha Baba yetu, Mzee Paulo
Kilaini, ambacho nimejulishwa kuwa kilitokea asubuhi siku ya Alhamisi, tarehe 3 Aprili
2014 katika Hospitali ya Mbweni, Dar Es Salaam.”
Ameongeza Rais Kikwete:“Mzee
Kilaini alikuwa mpenda maendeleo na siku zote alikuwa mstari wa mbele katika kusaka
maendeleo ya jamii yake na hasa hasa atakumbukwa kwa juhudi zake kubwa katika maendeleo
ya elimu. Aidha, ni dhahiri kuwa Mzee Kilaini ametuacha wakati busara zake zikiwa
zinahitajika zaidi katika jamii yetu”.
Amesisitiza Rais:“Baba Askofu, najua
kuwa kwako wewe na familia nzima ya Mzee Paulo Mutegeki Kilaini hiki ni kipindi kigumu.
Hivyo, nawatakieni rehema za Mwenyezi Mungu, awape uvumilivu na subira huko mkielewa
kuwa niko nanyi wakati wote wa msiba kwa sababu msiba huu pia ni msiba wangu. Aidha,
naungana nanyi katika kumwomba Mwenyezi Mungu aiweke peponi roho ya Marehemu Mzee
Paulo Mutegeki Kilaini. Amina.”