2014-04-04 09:01:56

Tumekuja kusali na kuteta na Baba Mtakatifu Francisko!


Askofu Tarcisius Ngalalekumtwa, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania katika mahojiano maalum na Radio Vatican anabainisha kwamba, hija ya kitume inayofanywa sasa na Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania kuanzia tarehe 4 hadi tarehe 7 Aprili 2014 ni utaratibu wa kawaida kwa Kanisa Katoliki. Hii ni hija ambayo walau hufanyika kila baada ya miaka mitano, ili kuweza kuonana, kusali na kuzungumza na Khalifa wa Mtakatifu Petro. RealAudioMP3

Hii ni nafasi ya kusali pia kwenye makaburi ya miamba wa imani: Mtakatifu Petro na Mtume Paulo, mwalimu wa mataifa. Hawa ni mashahidi wa kazi ya utangazaji wa Habari Njema ya wokovu, ambayo Yesu alitaka iendelezwe duniani kote. Hii ni nafasi pia kwa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania kutoa taarifa ya maisha na utume wa Kanisa nchini Tanzania kama sehemu ya mchakato wa kukuza na kudumisha umoja na mshikamano wa kidugu na imani.

Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania anasema kwamba, hii ni fursa ya kuwashirikisha viongozi wa Kanisa: furaha, matumaini na wasi wasi la Kanisa Katoliki nchini Tanzania. Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania linaendelea kusukuma mbele mchakato wa kuwatangaza Sr. Bernadetha Mbawala na Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, Baba wa Taifa kuwa ni kati ya Wenyeheri.

Askofu Ngalalekumtwa anasema, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere ni mfano wa mtu ambaye kama kiongozi mkuu wa taifa, alijitahidi kuzingatia majukumu yake, akajikita katika hekima, heshima, busara na upendo kwa wote bila ubaguzi. Chimbuko la utekelezaji wa majukumu yote haya na maisha yake adili ni imani kwa Kristo na Kanisa lake.

Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania linasema, haya ni mambo yanayowatia moyo katika shida na mahangaiko yao; wakati wa mashambulizi, dhuluma za kidini na misigano ya kijamii, kwa kutambua kwamba, Mwenyezi Mungu bado anawataka Maaskofu kuendelea kuwa waaminifu kwa Kristo na Kanisa lake. Wamefika kusali kwenye makaburi ya miamba wa imani, ili waendelee kutiwa nguvu ya kuwa ni mashahidi wa Kristo nchini Tanzania kwa kutambua kwamba, Mwenyezi Mungu ana huruma na mapendo na ataweza kuwasikiliza.

Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania, linawaalika kwa namna ya pekee waamini na watanzania wote kutubu na kumwongokea Mungu ili waweze kuponywa katika mapungufu yao na kupata maisha mapya pamoja na kukumbatiwa kwa upendo, wao wakionesha moyo wa toba na majuto.







All the contents on this site are copyrighted ©.