2014-04-03 14:35:54

Waziri mkuu wa Cape Verde akutana na kuzungumza na Papa Francisko mjini Vatican


Baba Mtakatifu Francisko, Alhamisi tarehe 3 Aprili 2014 amekutana na kuzungumza na Bwana Josè Maria Pereira Neves, Waziri mkuu wa Cape Verde, ambaye pia alipta fursa ya kukutana na kuzungumza na Kardinali Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican aliyekuwa ameambatana na Askofu mkuu Dominique Mamberti, Katibu mkuu wa mambo ya nchi za nje na ushirikiano wa kimataifa.

Ujumbe kutoka Cape Verde umeridhia pia makubaliano ya ushirikiano kati yake na Vatican, yanayotambua Kanisa Katoliki kisheria. Itakumbukwa kwamba, makubaliano haya yalitiwa sahihi kunako tarehe 10 Juni 2013.

Bwana Jorge Borges, Waziri wa mambo ya nchi za nje wa Cape Verde ameongoza ujumbe wa nchi yake, wakati ujumbe wa Vatican uliongozwa na Askofu mkuu Dominique Mamberti. Itifaki hii inaimarisha uhusiano kati ya nchi hizi mbili. Kuanzia sasa Jumapili itakuwa ni Siku ya Mapumziko kitaifa. Serikali italinda na kuhifadhi maeneo ya Ibada, ndoa inayofungwa na Kanisa kwa sasa inatambuliwa kisheria. Shule, taasisi na vyuo vikuu vinatambuliwa kisheria. Kanisa limepewa fursa ya kufundisha dini shuleni pamoja na kuendelea kutoa huduma za kijamii kwa maskini na wale wanaosukumizwa pembezoni.

Pamoja na mambo mengine, itifaki hii inaliwezesha Kanisa Katoliki nchini Cape Verde kutoa huduma za kichungaji katika vikosi vya ulinzi na usalama, hospitalini pamoja na kushughulia masuala ya kodi na mali ya Kanisa. Itifaki hii imeanza kutumika rasmi baada ya kuridhiwa na pande zote mbili.







All the contents on this site are copyrighted ©.