2014-04-03 08:09:44

Jengeni na kuimarisha misingi ya haki, amani na upatanisho, vita haina mashiko tena!


Kardinali Peter Turkson, Rais wa Baraza la Kipapa la haki na amani, hivi karibuni kwa niaba ya Baba Mtakatifu Francisko alifanya hija ya kichungaji nchini Sudan ya Kusini, ili kuonesha mshikamano wa upendo kutoka kwa Mama Kanisa wakati huu Wananchi wa Sudan ya Kusini wanapokabiliana na hali ngumu ya maisha kutokana na vita ya kikabila na machafuko ya kisiasa nchini humo. Vita ya wenyewe kwa wenyewe nchini Sudan imepelekea zaidi ya watu 1000 kupoteza maisha yao na wengine zaidi 150, 000 kuyakimbia makazi yao. RealAudioMP3

Akihojiwa hivi karibuni, Kardinali Turkson anasema, hija hii ya kitume ni kielelezo cha mshikamano wa dhati kati ya Kanisa la kiulimwengu na Kanisa mahalia. Kardinali Turkson, mwanzoni alipanga pia kutembelea wananchi wa Jamhiri ya Afrika ya Kati, lakini haikuwezekana kutokana na sababu zilizokuwa nje ya uwezo wake. Mashambulizi yanayoendelea huko Afrika ya Kati yasichukuliwe kuwa ni vita kati ya Waislam na Wakristo, bali changamoto kwa wananchi Barani Afrika kudumisha utamaduni wa kuheshimiana na kuthaminiana hata katika tofauti zao za kidini, kiimani, kikabila na kisiasa na pamoja walenge kutafuta ustawi, mafao na maendeleo ya wengi.

Kwa miaka mingi Waislam na Wakristo wamekuwa wakiishi kwa amani, utulivu na mapendo, lakini tabia ya misimamo mikali ya imani, inapelekea misingi ya haki, amani, upendo na mshikamano wa kitaifa kuanza kuyumba sehemu mbali mbali za Bara la Afrika. Kumbe, kuna haja ya kushikamana kwa pamoja ile kujenga Jamii inayoheshimiana na kuthaminiana.

Akizungumzia kuhusu mashambulizi yanayofanywa na Kikundi cha Kigaidi cha Boko Haram nchini Nigeria, Kardinali Turkson anabainisha kwamba, kadiri ya taarifa alizonazo kutoka kwa Maaskofu Katoliki nchini Nigeria, tatizo la Boko Haram ni tete kwani linaungwa mkono na baadhi ya wanasiasa, kuna chochoko choko za kidini zinazoona kwamba, utamaduni kutoka katika Nchi za Magharibi ni haramu na kwamba, unapaswa kupingwa kwa nguvu zote sanjari na kukataa kuridhia mfumo wa elimu kutoka katika Nchi za Magharibi.

Ni kweli kwamba, dini zinaweza kuchangia katika ustawi na maendeleo ya wananchi, lakini si kwa njia ya mtutu wa bunduki. Watu wanapaswa kutambua na kuheshimu mafundisho ya dini zao ili waweze kweli kuwa ni wajenzi wa misingi ya haki, amani, upendo na upatanisho wa kweli. Waamini wa dini mbali mbali wasikubali kutumiwa na wanasiasa kusababisha kinzani na vurugu kwa ajili ya mafao ya wanasiasa hawa, kwani watakaoumia si wanasiasa bali wananchi wasiokuwa na hatia.

Watu watambue kwamba, kwa njia ya mtutu wa bunduki hata kile kiwango kidogo cha maendeleo kilichokuwa kimefikiwa kitaathirika, kumbe kuna haja ya kujenga na kudumisha utamaduni wa majadiliano kama njia ya kutafuta suluhu ya migogoro ya kisiasa, kijamii, kidini na kiuchumi. Watu wazungumze wakiongozwa na ukweli, haki na mafao ya wengi.

Udini na Ukabila ni sumu ya maendeleo ya wengi, watu wasiendekeze mambo haya, bali wawe ni wajenzi wa mshikamano wa kitaifa kwa kutambua kwamba, tofauti zao si kwa bahati mbaya, bali ni mpango wa Mungu kwa ajili ya watu wake. Viongozi wa kisiasa na Kiserikali wajifunze kuheshimu Katiba ya Nchi ambayo kimsingi ni Sheria Mama, kwani tatizo la kutaka kupindisha Katiba ndicho chanzo kikuu cha kinzani na migogoro ya kisiasa, kijamii na kidini katika nchi mbali mbali Barani Afrika.

Inasikitisha kuona kwamba, wakati wa kampeni za chaguzi nyingi Barani Afrika watu wanatumia kiasi kikubwa cha fedha, kumbe wanaposhindwa katika uongozi, wanatafuta njia za mkato za kutaka kuingia madarakani kwa nguvu, jambo ambalo ni kinyume kabisa cha misingi ya demokrasia na utawala wa sheria.

Kardinali Peter Turkson, Rais wa Baraza la Kipapa la haki na amani anasema, ujumbe mzito aliwaachia wananchi wa Sudan ya Kusini ni matumaini yanayojengeka katika misingi ya usawa, uhuru wa kweli na udugu. Haya ni mambo yanayohitaji muda mrefu ili kuweza kumwilishwa katika uhalisia wa maisha ya wananchi wa Sudan ya Kusini.

Ni matumaini yatakayowawezesha kuwa na maisha yenye furaha, amani na utulivu, kila mwananchi akijitahidi kutekeleza dhamana na wajibu wake ndani ya Jamii husika. Watu wajifunze kuheshimiana na kuthaminiana kama ndugu na kamwe wasitazamane kama adui. Serikali zitekeleze dhamana na wajibu wake wa kulinda utawala wa sheria, amani, utulivu na maendeleo ya wengi.

Imeandaliwa na
Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.