Mkutano mkuu wa Maaskofu Katoliki Italia kufunguliwa na Papa Francisko, Mei, 2014
Baba Mtakatifu Francisko anatarajiwa kufungua mkutano mkuu wa Baraza la Maaskofu Katoliki
Italia, utakaoadhimishwa mwezi Mei mwaka huu. Maaskofu wanamshukuru Baba Mtakatifu
kwa kumteua Askofu Nunzio Galantino kuwa Katibu mkuu wa Baraza la Maaskofu Katoliki
Italia kwa kipindi cha miaka mitano na kwamba, atakuwa ni chombo muhimu kitakachowaunganisha
Maaskofu katika kudumisha na kukoleza udugu, ushiriki, usikilizaji na majadiliano
ya kweli na uwazi kati ya Maaskofu.
Hii ni sehemu ya tamko kutoka Kamati kuu
ya Baraza la Maaskofu Katoliki Italia baada ya kuhitimisha kikao chake hivi karibuni
hapa mjini Roma. Maaskofu wamekazia umuhimu wa kuonesha mshikamano wa upendo na udugu
kwa wale wasiokuwa na fursa za ajira; athari zinazotokana na myumbo wa uchumi kimataifa
ambao umepelekea familia nyingi kujikuta zinakabiliana na hali ngumu ya maisha na
mpasuko katika maisha ya ndoa na familia. Wananchi wengi wa Italia kwa sasa wanaelemewa
na umaskini wa hali na kipato; umaskini wa maadili, utu wema na maisha ya kiroho.
Makundi yote haya hayana budi kusaidiwa kikamilifu katika safari ya maisha yao ya
kiutu na kiroho.
Kamati kuu ya Baraza la Maaskofu Katoliki Italia limejadili
kwa kina na mapana jinsi ya kupambana na mmong'onyoko wa tunu msingi za kimaadili
na utu wema; rushwa na ubadhirifu wa mali ya umma; sera za kisiasa zinazokwenda kinyume
na ubinadamu. Kuna haja wanasema Maaskofu kuvuka vikwazo vinavyokwamisha maisha ya
ndoa na familia; uhuru wa wazazi na walezi kuchagua mfumo wa elimu wanaoupenda kwa
ajili ya ustawi na maendeleo ya watoto wao. Kumbe, kuna haja ya kusimama kidete kulinda
na kutetea utu na heshima ya binadamu, kwa kuwasaidia wale walioathirika wakiwa njiani
kuelekea Yeriko kutoka na ubinafsi wa kutupwa.
Baraza la Maaskofu Katoliki
Italia katika mkutano wake, limekazia umuhimu wa Shule za Kikatoliki na mchango wake
katika ustawi na maendeleo ya wengi. Wamejadili pia kuhusu maisha ya kitawa kwa kuangalia
mambo msingi na taratibu zinazoweza kutumiwa na Kanisa Katoliki nchini Italia. Wamefanya
tafakari ya kina kuhusu Hati ya Maadhimisho ya Siku ya 47 ya Juma la Kijamii nchini
Italia na kuridhika kuhusiana na mwelekeo na katekesi yake na kwamba, hati hii itajadiliwa
wakati wa mkutano mkuu wa Baraza la Maaskofu Katoliki Italia, utakaofanyika mwezi
Mei, 2014.