Watanzania wamkumbuka Marehemu John Tuppa! Mtu wa watu!
Waziri mkuu wa Tanzania Mizengo Pinda ameongoza viongozi mbalimbali na mamia ya wakazi
wa Mkoa wa Dodoma kuuaga mwili wa aliyekuwa Mkuu wa mkoa wa Mara ambaye alifariki
dunia ghafla Machi 25, 2014 akiwa ziarani wilayani Tarime. Shughuli ya kuuaga rasmi
mwili wa marehemu John Gabriel Tuppa kwa wakazi wa mji wa Dodoma ilifanyika mchana
Ijumaa, Machi 28, 2014 kwenye viwanja vya Mwalimu Nyerere ambako ibada ya kumwombea
marehemu ilifanyika. Baadaye mchana, mwili wake ulisafirishwa kwenda wilayani Kilosa,
mkoani Morogoro kwa mazishi. Akizungumza na waombolezaji hao kabla ya kutoa heshima
za mwisho, Padri Chesco Msaga, Makamu Askofu Jimbo Katoliki la Dodoma ambaye aliongoza
ibada hiyo, alisema Mungu aliwaumba wanadamu ili wampende na wamtumikie na kwamba
marehemu Tuppa alilitimiza jambo hilo vilivyo. Alisema wakati wa uhai wake, Bw.
Tuppa alipenda haki na popote alipokwenda alitetea haki za wanyonge. “Sote ni mashahidi
wa jinsi alivyopenda watu na jinsi alivyowatumikia watu. Alikuwa mnyenyekevu, aliwasikiliza
wengine na alithamini michango ya wengine. Na sisi tunapaswa kuiga hilo,” alisema. Naye
Dk. Right Mmbaga, akitoa salamu za rambirambi kwa niaba ya Baraza la Wazee la Dodoma
Mjini alisema: “Wale watumishi ambao bado wako kazini na walipata nafasi ya kufanya
kazi na Bw. Tuppa, wajifunze kutoka kwake na wafuate nyayo zake kama njia ya kumuenzi.” Naye
Naibu Waziri wa Fedha, Bw. Mwigulu Nchemba, akitoa salamu kwa niaba ya Katibu Mkuu
wa CCM, alisema Chama cha Mapinduzi kimempoteza kamisaa makini sana aliyekuwa mstari
wa mbele katika utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya chama hicho. Mwenyekiti wa
Bodi ya Mamlaka ya Ustawishaji Makao Makuu (CDA), Bw. William Lukuvi aliwaasa wakazi
wa Dodoma kuenzi mambo ambayo Bw. Tuppa aliwafanyia wakati akiwa Mkuu wa Wilaya ya
Dodoma hata kama walikuwa hawayaoni. “Alikuwa na upeo wa kufanya kazi kwa kasi
lakini kwa utulivu. Wakati tumeanza naye kazi hapa Dodoma mwaka 2006, kulikuwa na
shule sita tu za sekondari lakini katika kipindi cha miaka miwili alifanikisha kusimamia
ujenzi wa shule za sekondari 30,” alisema Bw. Lukuvi ambaye wakati huo alikuwa Mkuu
wa Mkoa wa Dodoma. Akizungumza kwa niaba ya viongozi wa Makanisa ya mkoa wa Dodoma,
Askofu Dk. Yohana Masinga alisema viongozi hawajui kwamba wakishateuliwa, wao ni watumishi
wa Mungu kwa sababu wanawaongoza watu walioumbwa kwa sura na mfano wa Mungu.. Akinukuu
Neno la Mungu kutoka Waraka kwa Waebrania sura ya 13 aya ya 7, linalosema wakumbukeni
waliokuwa wakiwaongoza, ichunguzeni miisho ya mwenendo wao na iigeni imani yao, Askofu
Masinga aliwataka wote waige mfano wa utendaji kazi wa Bw. Tuppa. “John Tuppa alikuwa
ni mtendaji na Kanisa limempoteza mtu makini. Ninawaomba viongozi wa nchi hii waige
mfano wa John Tuppa. John Tuppa awe ni mfano kwao, na wafanye hivyo kwa ukombozi wa
nchi yetu,” alisema. Bw. Tuppa anatarajiwa kuzikwa Jumamosi, Machi 29, 2014 wilayani
Kilosa. Alizaliwa Januari mosi, 1950. Amewahi kuwa Mkuu wa Wilaya za Chunya, Mwanga,
Bukoba, Muleba na Dodoma kabla ya kuteuliwa kuwa Mkuu wa Mkoa wa Mara mwaka 2011.
Ameacha mke na watoto watano.