2014-03-28 08:17:51

Tafakari ya neno la Mungu, Jumapili ya Nne ya Kipindi cha Kwaresima


Niko nawe tena katika kipindi tafakari masomo Dominika ya IV ya Kipindi cha Kwaresima, ambapo tunaalikwa kuwa watu wa mwanga. Katika somo la kwanza tunakutana na uteuzi wa kiongozi atakayeongoza taifa la Israeli. RealAudioMP3

Mpendwa mwana wa Mungu, jambo hili linatokea miaka 1000 kabla ya Kristu wakati ambao Waisraeli walikuwa katika shida na taabu. Ili kuweza kuondokana na taabu hizi walilazimika kutafuta kiongozi atakayewasaidia kuwaongoza ili waweze kupata ushindi toka Wafilistini. Kwa njia ya Samueli Mungu anaonesha kijana mmoja toka Betlehem katika ukoo wa Yese, ambaye atapakwa mafuta kwa ajili ya kuwa mfalme wao.

Basi Nabii atakwenda mpaka Betlehem na kumwambia habari hii Yese ya kwamba mmojawapo wa wanawe amechaguliwa na Mungu kuongoza taifa la Israeli. Yese anapokea habari hii kwa furaha kuu. Katika furaha hiyo, Yese anafikiri na kuona kwa mtizamo wake, kuwa mtoto huyu atakuwa ELIABU. Katika hali ya kawaida, Eliabu alikuwa mrefu na mzuri, tena alikuwa mtoto wa kwanza. Samweli anavutiwa na sura ya Eliabu, lakini Mungu anasema hapana!

Kwa hapana ya Mungu, Yese atalazimika kuwaleta watoto wake wote isipokuwa Daudi aliyekuwa machungani! Mpendwa msikilizaji, kati ya watoto hawa walioletwa hakukuwa na aliyechaguliwa na Mungu na hivi Samueli akamwambia akamlete Daudi. Yese kwa kuamuliwa amlete Daudi alisema bado Daudi ni mdogo kwa utume ambao ni mkubwa namna hii! Lakini Nabii atasisitiza kuwa huyu ndiye chaguo la Mungu.

Mpendwa msikilizaji, katika uchaguzi huu tunagundua kuwa njia za Mungu na njia zetu ni tofauti kabisa. Fikiria kwa kuchagua taifa la Israeli liwe taifa teule aliacha taifa imara kiuchumi yaani Babilonia, akaacha Misri lililokuwa taifa lenye ufundi wa hali juu na lenye watu wa dini, (Deut, 7:7-8). Ni katika mlengo ule ule katika AJ Bwana atawachagua maskini, wadhambi, wanaoteswa, na wanaotengwa kwa ajili ya ufalme wake. Kumbuka pia alipozaliwa watu wa kwanza kushuhudia utukufu wake ni wachungaji waliokuwa kondeni. Mpendwa msikilizaji, ndiyo kusema hatuna mamlaka ya kuingilia mpango wa Mungu, ni vema siku zote tukajisalimisha katika yeye kadiri ya mapenzi yake.

Katika somo la Pili Mtakatifu Paulo anawaandikia Waefeso akisema, kwa njia ya ubatizo wametwaliwa toka giza na kuingizwa katika mwanga. Kwa tendo la kuingizwa katika utawala wa mwanga, wanaalikwa kuishi na kutenda matendo ya mwanga na kuachana na matendo ya aibu. Anasonga mbele akisema lazima kukemea matendo yaliyo ya aibu tena katika uwazi na kuyapatilizia mbali.

Katika Injili tunakutana na picha ya kipofu anayeponywa na Bwana. Jambo la msingi na fundisho la Bwana ni kwamba yeye amekuja kuwaondolea watu upofu wao na hasa upofu wa kiroho. Tunaona kabla ya tendo hilo jema, wafuasi wake watamwuliza wakisema: Bwana, hivi ni nani kati ya mtoto kipofu na wazazi wake aliyetenda dhambi mpaka mtoto yuko hivi?

Wanauliza swali hili kwa sababu kulikuwa na imani kwamba Mungu huwaadhibu wenye dhambi na kuwarehemu wema! Ndiyo kusema magonjwa na mikosi ilikuwa ni tokeo la dhambi! Aidha, aliyezalwa katika shida kama hizo alidhihirisha kuwa dhambi ilitendwa na wazazi pamoja na mababu. Mpendwa mwana wa Mungu, kufikiri hivi ni kinyume cha mapendo ya Mungu kwa watu, kwa hakika Mungu hajui kuadhibu bali kupenda tu. Ndiyo kusema shida zilizopo zinakuja kwa sababu ya uzembe wetu na hivi lazima tutafute suluhisho na namna ya kukabiliana nazo.

Katika sehemu ya pili ya Injili tunaona sasa ukamilifu wa kile alichokifundisha, yaani anakiweka katika matendo. Katia kutenda mwujiza wa kumfanya kipofu aone tena, anatema mate chini na kufanya tope ambalo atampaka kipofu. Baada ya hilo anamwambia nenda kanawe katika birika ya Siloamu na kwa kufanya hivyo kipofu anaona! Mpendwa msikilizaji, kuna nini katika matendo haya? Mambo yako hivi kwa sababu watu wa wakati huo waliamini katika pumzi kuwako na roho na katika mate kulijaa nguvu ya mtu.

Ndiyo kusema Bwana anatumia alama zilezile kutenda kazi yake ya kuleta uhuru kwa kipofu. Bwana haishii tu katika alama hizi za mwanzo bali anamwambia nenda ukanawe katika Siloamu, ndiyo kusema anamtuma. Hapa tunaona Bwana aliyetumwa na Mungu anamwalika mtu kuja kwake ili apate maji ya uzima, maji yanayoponyesha kama alivyomwahidia mwanamke msamaria, na kisha kwenda kutangaza habari njema ya furaha.

Baada ya tendo hili la uponyaji kipofu ataulizwa na watu mbalimbali kuhakikisha ni kwa nguvu ya nani amepona. Wa kwanza ni majirani zake ambao wanajiuliza ni yeye au ni mwingine na baadaye watampeleka kwa Mafarisayo ambao watamlalamikia Bwana badala ya kumsifu, ati kwa sababu alitenda kazi hiyo wakati wa Sabato, na kwa jinsi hiyo Bwana hakutoka kwa Mungu. Katika hili wengine walisema lakini inawezekanaje mwenye dhambi afanye mwujiza huu?

Kwa majirani kipofu atasema mimi ndiye na wala si mwingine. Kwa Mafarisayo atasema yakuwa aliyeniponya ni Nabii. Mpendwa msikilizaji, katika kuendelea kutafuta ukweli, wenye madaraka watawaendea wazazi wake na kuwauliza na wazazi kwa woga wa kutengwa watasema kamwulizeni yeye mwenyewe kwa kuwa ni mtu mzima. Wenye mamlaka watamrudia aliyekuwa kipofu wakitaka akane ukweli na yeye atawaambia ninachojua ni kwamba nilikuwa kipofu na sasa ninaona. Ndugu huyu aliendelea kutetea ukweli huo kwa furaha mpaka mwisho.

Mpendwa, katika hili twajifunza kuwa wakweli na kuwa wenye furaha daima, na hivi kusimamia imani na matendo makuu ya Mungu. Ndiyo kusema furaha na neema za Mungu tulizozipokea kwa njia ya ubatizo na kipaimara twapaswa kuzitunza mpaka mwisho wa nyakati. Tena, katika safari ya kulinda imani kutakuwa na wakati wa furaha na mateso, jambo kuu ni kuweka tumaini katika yeye aliyetuponya.

Mpendwa ninakutakia furaha na matumaini katika maisha yako daima ukimtanguliza Mungu na kwa nguvu zake kukua na kusimamia imani uliyoipokea kama zawadi toka kwake.

Tumsifu Yesu Kristo. Tafakari hii imeletwa kwako na Padre Richard Tiganya C.PP.S.








All the contents on this site are copyrighted ©.