2014-03-28 08:31:07

Jitahidini kuchuchumilia utakatifu!


Utakatifu ni changamoto na mwaliko kwa waamini wote na wala si kwa ajili ya watu wachache waliobahatika katika hija ya maisha yao. Hii inatokana na ukweli kwamba, Mwenyezi Mungu ni Mtakatifu, kumbe hata waamini wanapaswa kuchuchumilia utakatifu wa maisha, kila mtu kadiri ya wito, maisha na utume wake ndani ya Kanisa. Waamini wanapaswa kumfuasa Yesu Kristo ambaye alikuwa ni fukara, mnyenyekevu aliyethubutu kuubeba Msalaba, ili kuwashirikisha waamini katika utukufu wake. RealAudioMP3

Hivi ndivyo Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican wanavyoandika katika Hati ya Mtaguso mkuu kuhusu Kanisa, Lumen Gentium, yaani Mwanga wa Mataifa. Huu ni mwelekeo mpya uliobainishwa na Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican. Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI katika Katekesi yake ya tarehe 13 Aprili 2011 anawaalika waamini kuitafuta na kuanza hija inayoelekea katika utakatifu wa maisha kwa kutambua kwamba, maisha matakatifu si juhudi na nguvu za mtu binafsi, bali ni baraka na neema inayotolewa na Mwenyezi Mungu ambaye ni Mtakatifu wa watakatifu anayewawezesha waamini kuwa ni watakatifu. Hii ni kazi ya Roho Mtakatifu anayemwalika mwamini kutoka katika undani wa maisha yake kwa kumkirimia neema inayomletea toba na wongofu wa ndani.

Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican unakumbusha kwamba, Wafuasi wa Kristo wanaitwa kumfuasa Kristo kwa vile wameitwa na Mwenyezi Mungu kadiri ya mpango na neema inayowahesabia kuwa haki mbele ya Mwenyezi Mungu. Kwa njia ya imani katika Ubatizo, Wakristo wanafanyika kuwa ni Watoto wa Mungu wanaoshirikishwa utukufu, ukuu na umungu wa Kristo. Wakristo wanashiriki katika Fumbo la Pasaka kwa njia ya neema inayobubujika kutoka kwa Roho Mtakatifu.

Kwa njia ya Ubatizo anasema Mtakatifu Paulo, mwamini ameifia dhambi, akazikwa na kufufuka pamoja na Kristo, kiasi kwamba, maisha ya Mkristo yanapaswa kufungamana na Kristo, tayari kuanza hija inayomwezesha mwamini kutembea katika mwanga wa Kristo Mfufuka. Lakini anakumbusha Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI, Mwenyezi Mungu anapenda kuheshimu uhuru wa kila binadamu. Anamtaka mwamini mwenyewe kukubali na kushiriki katika mpango wake kwa njia ya toba na wongofu wa ndani, ambao mwamini anakirimiwa kama zawadi kutoka kwa Roho Mtakatifu. Utashi wa binadamu hauna budi kuenda sanjari na utashi wa Mungu, ili hatimaye, kufikia utakatifu.








All the contents on this site are copyrighted ©.