Baba Mtakatifu Francisko, Ijumaa tarehe 28 Machi 2014 amekutana na kuzungumza na washiriki
wa kozi maalum iliyokuwa imeandaliwa na Baraza la Toba ya Kitume, iliyowashirikisha
Mapadre wapya na Mashemasi kama sehemu ya majiundo makini kwa waungamishaji wa baadaye,
kwa kutambua thamani ya utume huu ambao wanakabidhiwa na Mama Kanisa.
Baba
Mtakatifu anawaalika washiriki wa kozi hii kuhakikisha kwamba, wanatumia uzoefu, mangamuzi
na ugunduzi makini ili kulisaidia Kanisa na waungamishaji kutekeleza utume wa huruma
ya Mungu ambao ni muhimu sana. Wahudumu wa Sakramenti ya Upatanisho watambue kwamba,
mhusika mkuu katika Sakramenti ya Upatanisho ni Roho Mtakatifu anayemkirimia mwamini
maisha mapya yanayobubujika kutoka kwa Kristo Mfufuka. Waungamishaji wanachangamotishwa
kuwa ni watu wa Roho Mtakatifu, mashahidi na watangazaji makini na wenye furaha juu
ya ufufuko wa Kristo, mambo yanayojidhihirisha katika Sakramenti ya Upatanisho.
Padre
muungamishaji awapokee waamini kwa upendo na huruma inayobubujika kutoka kwa Kristo
mwenyewe. Wao ni Mahakimu na Waganga wa mioyo ya waamini, kwa kuponya na kuwaondolea
watu dhambi zao.
Baba Mtakatifu anasema, Sakramenti ya Upatanisho inamkirimia
mwamini maisha mapya pamoja na kuboresha neema ya Sakramenti ya Ubatizo, mwaliko wa
kuwapatia waamini neema hii kwa moyo mkuu. Mapadre wawahudumie waamini wao kwa kuhakikisha
kwamba, wanatenga muda wa kutosha sanjari na kuwa na maisha bora ya kiroho, kwani
huruma ni kiini cha Injili.
Ni mwaliko kutoka kwa Mwenyezi Mungu anayempenda
mdhambi na kumwalika kutubu na kuongoka. Baba Mtakatifu anakiri kwamba, waamini wanapata
shida katika kukimbilia kiti cha maungamo ili kuungama dhambi zao kwa binadamu mwenzao.
Kutokana na ukweli huu, kuna haja ya kuhakikisha kwamba, Mapadre hawawi vikwazo kwa
waamini katika kukimbilia huruma na upendo wa Mungu.
Mapadre wawe na busara
katika kutoa Sakramenti ya Upatanisho, wawe wasikivu na kuwasaidia waamini kuweza
kujipatanisha na Mungu. Kiti cha maungamo iwe ni fursa ya kuonja msamaha na huruma
ya Mungu. Baba Mtakatifu anasema, Sakramenti ya Upatanisho ni zawadi ya Kristo kwa
Kanisa lake, ili kuwawezesha waamini kupokea huruma ya Mungu.
Kumbe, kuna
haja ya kuhakikisha kwamba, Sakramenti ya Upatanisho inaadhimishwa kikamilifu, kwani
ni chemchemi ya huruma na wokovu. Mapadre wajipange barabara ili kutoa nafasi kwa
waamini kuungama dhambi zao, wakitambua kwamba, uaminifu unazaa matunda mwengi. Nyumba
za kitawa zijitahidi kuwa na Mapadre ambao wanaweza kuungamisha watu kwa muda mrefu
zaidi. Baba Mtakatifu anawatakia Mapadre wote neema na baraka ya kutambua umuhimu
wa Sakramenti ya Upatanisho.