2014-03-27 15:34:32

Rais Obama akutana na kuzungumza na Papa Francisko mjini Vatican


Baba Mtakatifu Francisko siku ya Alhamisi tarehe 27 Machi 2014 majira ya asubuhi, amekutana na kuzungumza na Rais Barack Obama wa Marekani pamoja na ujumbe wake. Baadaye, Rais Obama alikutana pia na Kardinali Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican aliyekua ameambatana na Askofu mkuu Dominique Mamberti, Katibu mkuu wa mambo ya nchi za nje na ushirikiano wa kimataifa mjini Vatican.

Katika mazungumzo ya viongozi hawa wawili, wamebadilishana mawazo kuhusu masuala tete yanayoendelea kujitokeza katika Jumuiya ya Kimataifa na kwamba; maeneo yanayokabiliana na vita pamoja na kinzani za kijamii yanapaswa kuheshimu haki msingi za binadamu sanjari na haki za kimataifa; majadiliano yapewe kipaumbele cha pekee katika kufikia suluhu ya kinzani hizi.

Rais Obama pamoja na Baba Mtakatifu wamegusia pia ushirikiano kati ya Kanisa na Serikali pamoja na kukiri kwamba, Kanisa limekuwa mstari wa mbele katika kuchangia mafao ya wengi na kwamba, uhuru wa kidini, maisha, uhuru wa kidhamiri na mabadiliko katika sheria za uhamiaji ni mambo yanayopaswa kupewa kipaumbele cha pekee katika utekelezaji wake.

Kwa pamoja, viongozi hawa wamekubaliana kimsingi kwamba, kuna haja ya kusimama kidete kupambana kufa na kupona dhidi ya biashara haramu ya binadamu ulimwenguni.







All the contents on this site are copyrighted ©.