Familia ni mhimili mkuu wa maendeleo endelevu ya binadamu!
Huduma makini kwa familia inayojikita katika: akili, ujasiri na upendo wa dhati, ndiyo
mambo msingi yanayobainishwa na Askofu mkuu Vincenzo Paglia, Rais wa Baraza la Kipapa
la Familia wakati wa kuzindua maandalizi rasmi ya Maadhimisho ya Siku ya Nane ya Familia
Kimataifa itakayoadhimishwa Jimbo kuu la Philadelphia, Marekani kuanzia tarehe 22
hadi tarehe 27 Septemba 2015.
Mama Kanisa anapenda kuweka mikaka makini inayojikita
katika ujasiri ili kukabiliana na changamoto zinazojitokeza katika maisha na utume
wa Familia ndani ya Kanisa na Jamii katika ujumla wake. Upendo wa dhati unapania kuvuka
vikwazo vilivyopo katika maisha ya ndoa na familia kwa kuzingatia Injili ya Familia
na Maisha ya mwanadamu.
Uzinduzi wa Maandalizi ya Maadhimisho ya Siku ya nane
ya Familia Kimataifa yamehudhuriwa pia na Askofu mkuu Charles Joseph Chaput, kutoka
Jimbo kuu la Philadelphia Marekani pamoja na ujumbe wake, watakaokuwa ni wenyeji wa
maadhimisho hayo. Hii ni fursa makini kwa Mama Kanisa kuweza kujikita zaidi katika
taalimungu ya maisha ya ndoa na familia; tasaufi na utakatifu wa maisha kati ya wanandoa;
Kanisa na Familia; Familia na Tamaduni mamboleo pamoja na changamoto zake; Familia
na tatizo la uhamiaji; Familia na Majadiliano ya kidini na kiekumene.
Hizi
ni kati ya changamoto msingi zinazopaswa kufanyiwa kazi na Mama Kanisa katika maisha
na utume wake kwa Familia, kwa kujikita katika mikakati thabiti na yenye akili, ujasiri
na upendo mkamilifu kwa maisha ya ndoa na familia. Mama Kanisa analionesha hili kwa
kuitisha Sinodi maalum na ile ya kawaida kwa ajili ya Familia, kwa kutambua kwamba,
Baba Mtakatifu Francisko ameendelea kutoa kipaumbele cha pekee katika maisha ya ndoa
na familia ndani ya Kanisa, kama ilivyojionesha katika kikao cha Baraza la Makardinali
kilichohitimishwa hivi karibuni hapa mjini Vatican.
Maadhimisho ya Siku ya
Nane ya Familia Kimataifa huko Philadelphia, Marekani ni sehemu ya mchakato wa Mama
Kanisa katika kutafuta ufumbuzi wa changamoto zinazojitokeza katika maisha ya ndoa
na familia. Familia ni tema inayojadiliwa pia kwenye Umoja wa Mataifa, kwani Mwaka
2014, Jumuiya ya Kimataifa inaadhimisha Mwaka wa Familia. Kumbe hili ni tukio ambalo
linalishirikisha Kanisa Katoliki nchini Marekani, lakini pia lina mwelekeo mpana zaidi
kwani uwepo wa Baba Mtakatifu Francisko, utakoleza mchakato wa kutafuta ufumbuzi wa
changamoto za kifamilia.
Huu ni mwaliko anasema, Askofu mkuu Paglia kwa Jumuiya
ya Kimataifa kushikamana kwa pamoja ili kuweza kuipatia Familia kipaumbele cha pekee,
ili kujenga na kuimarisha udugu, upendo na mshikamano wa dhati kati ya binadamu, ili
kweli familia ya binadamu iweze kujisikia kuwa ni wamoja.
Askofu mkuu Chaput
amewasili mjini Vatican akiwa na ujumbe mzito wa wadau kutoka katika vyama vya kitume
vinavyojihusisha na maisha ya kifamilia pamoja na wanasiasa ambao kwa pamoja wanalenga
kufanikisha maandalizi na hatimaye, maadhimisho ya Siku ya Nane ya Familia Kimataifa.
Anasema, maadhimisho haya ni fursa ya neema na furaha kwa Kanisa zima kwa kutambua
kwamba, familia ni kikolezo makini cha maendeleo endelevu ya mwanadamu.
Kanisa
na Jamii kwa ujumla hawana budi kushirikiana kwa ajili ya kuboresha maisha ya familia,
kwa kutunga sera makini pamoja na kuyatafutia ufumbuzi matatizo yanayozikabili familia
nyingi duniani. Jimbo kuu la Philadelphia linaendelea kuboresha miundo mbinu na mahudhui
yatakayofanyiwa kazi wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Nane ya Familia Kimataifa.
Katika
uzinduzi wa maandalizi ya Maadhimisho ya Siku ya Familia Kimataifa, baadhi ya waamini
na wakereketwa wa maisha ya ndoa na familia kutoka Marekani, wametoa ushuhuda wao,
kuhusu umuhimu wa maisha ya ndoa na familia ndani na nje ya Kanisa, kwani familia
ni shule ya utakatifu, haki, amani, upendo na mshikamano wa dhati. Tunu msingi za
maisha ya kifamilia zikiboreshwa, dunia inaweza kuwa ni mahali pazuri zaidi pa kuishi.