2014-03-26 14:43:58

Endeleeni kusali ili Jumuiya za Waamini zisitindikiwe na Mapadre wema, watakatifu na wachapakazi


Sakramenti ya Ubatizo, Kipaimara na Ekaristi Takatifu ni Sakramenti ambazo zinamwingiza mtu katika Ukristo na kuwashirikisha watu hali ya kimungu kwa njia ya Yesu Kristo na hivyo kuwafungulia mlango wa wokovu. Huu ndio wito wa kwanza kabisa unaowashikamanisha wafuasi wote wa Kristo ndani ya Kanisa. Sakramenti ya Daraja Takatifu na Ndoa Takatifu ni Sakramenti za ushirika na kwa ajili ya wokovu wa watu wengine na zinachangia pia wokovu wa mtu binafsi kwa njia ya huduma kwa wengine na ujenzi wa Kanisa la Kristo

Ni utangulizi uliofanywa na Baba Mtakatifu Francisko wakati wa Katekesi yake, Jumatano, tarehe 26 Machi 2014 kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro, mjini Vatican pamoja na kuendelea kupembua Sakramenti ya Daraja Takatifu. Papa anasema, Daraja takatifu ni Sakramenti ambayo kwayo utume uliokabidhiwa na Kristo kwa mitume wake huendelea kutekelezwa katika Kanisa hadi mwisho wa nyakati: hivyo hii ni Sakramenti ya huduma ya kitume nayo ina ngazi kuu tatu: Uaskofu, Upadre na Ushemasi.

Baba Mtakatifu Francisko anasema wale walioteuliwa na kuwekwa wakfu wanaendeleza huduma ya Roho wa Kristo ndani ya nyakati na kuonesha uwepo wa Kristo ambaye ni Mwalimu na Mchungaji mwema. Makleri waliwekwa wakfu ni wakuu wa Jumuiya ya Kikristo wanaopaswa kutambua kwamba, wao ni wahudumu, kama Yesu mwenyewe alivyoonesha katika maisha na mafundisho yake, kwani Yeye alikuja si kwa ajili ya kuhudumiwa bali kuhudumia na kuyatoa maisha yake ili yawe ni fidia kwa wengi.

Padre anapaswa kuwa na upendo mkubwa kwa Kristo na Kanisa lake, kama vile ambavyo Kristo alilipenda Kanisa lake kiasi cha kujisadaka na kulitakatifuza, kwa njia ya Maji na Neno, ili kuonesha utukufu wa Kanisa pasi na mawaa. Padre anapaswa kujisadaka kwa akili na moyo wake wote bila hata ya kujibakiza. Hii ndiyo familia yake ambayo kamwe hapaswi kuibinafisha. Baba Mtakatifu anasema, Yesu Kristo ndiye mchumba pekee na mwaminifu wa Kanisa lake na yote ni mali yake!

Baba Mtakatifu anasema, maisha ya Kipadre ni mwaliko wa Padre kumwilisha ile zawadi iliyoko ndani mwake, aliyoipokea kwa njia ya Neno na kuwekewa mikono. Maisha ya Kipadre hayana budi kurutubishwa kwa njia ya Sala, Tafakari ya Neno la Mungu, Adhimisho la Fumbo la Ekaristi Takatifu pamoja na kupokea mara kwa mara Sakramenti ya Upatanisho, ili kujenga na kuimarisha upendo na mshikamano pamoja na Yesu, vinginevyo, Padre anaweza kujikuta akimezwa na malimwengu.

Padre atambue kwamba, daima anahimizwa kumwongokea Mwenyezi Mungu na kukimbilia upendo na huruma ya Mungu katika maisha yake; hapa ni mahali pa kuchota nguvu na mfano unaopaswa kutolewa kwa ndugu zake katika Jumuiya. Baba Mtakatifu anawaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema kusali kwa ajili ya kuwaombea wale wote wenye Daraja Takatifu katika Kanisa, lakini zaidi wale wanaokabiliana na hali ngumu ya maisha; watu ambao wako katika mchakato wa kutafuta tena upya wa maisha ya wito wao.

Baba Mtakatifu anawaomba waamini kuendelea kusali ili kamwe, Jumuiya za waamini zisitindikiwe na wachungaji wema na watakatifu, mintarafu Moyo wake mtakatifu. Wawe ni viongozi kadiri ya Maandiko Matakatifu, waaminifu kwa Kristo na Kanisa lake; makini katika huduma kwa binadamu, daima wakijitahidi kufuata mfano wa Kristo Mchungaji mwema, aliyethubutu kuwaosha miguu Mitume wake na hatimaye, akajimimina pale juu Msalabani kwa ajili ya wokovu wa ulimwengu.

Mwishoni, Baba Mtakatifu wakati akizungumza na mahuaji pamoja na wageni kutoka sehemu mbali mbali za dunia, ameendelea kuwahimiza waamini na watu wote wenye mapenzi mema kuendelea kujikita katika mchakato wa ujenzi wa misingi ya amani na mshikamano wa kidugu kati ya watu. Bikira Maria Mama wa Mungu ambaye, Kanisa limemsherehekea kwa kupashwa habari kuwa Mama wa Mungu, awasaidie vijana kuwa wasikivu wa utashi wa Mungu katika maisha yao kama alivyofanya Bikira Maria.

Wagonjwa wasikatishwe tamaa na magumu wanayokabiliana nayo katika hija yao ya maisha, kwani Mwenyezi Mungu hawezi kuwapatia Msalaba mkubwa unaozidi nguvu na uwezo wao. Wanandoa wapya wajenge maisha yao katika msingi wa Neno la Mungu.







All the contents on this site are copyrighted ©.