Watangazieni watu Injili ya Familia na Uzuri wake!
Ndoa na familia ni mada iliyokuwa inapembuliwa kwa kina na mapana na wanafunzi pamoja
na majaalimu wao kutoka sehemu mbali mbali za dunia, katika semina iliyoandaliwa na
Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Ulaya, (CCEE) kwa kushirikiana na Taasisi
ya Ndoa na Familia ya Yohane Paulo II hapa mjini Roma. Wajumbe wameangalia kwa umakini
mkubwa urithi ambao Mwenyeheri Yohane Paulo II ameliachia Kanisa katika mafundisho
yake kuhusu Ndoa na Familia.
Wajumbe wanasema kwamba, kuna utajiri mkubwa wa
Mafundisho ya Mwenyeheri Yohane Paulo II, kama yakitumika barabara yanaweza kuwa ni
msaada mkubwa katika kukabiliana na changamoto katika maisha ya ndoa na familia katika
ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia. Semina hii imeratibiwa
na Kardinali Lorenzo Baldiseri, Katibu mkuu wa Sinodi za Maaskofu Katoliki.
Wajumbe
wanasikitika kusema kwamba, kuna umati mkubwa wa waamini ambao hawafahamu kwa undani
Mafundisho ya Kanisa kuhusu Ndoa na Familia. Haya yamejidhihirisha hata katika majibu
ya maswali dododo kuhusu ndoa na familia kwa ajili ya Maadhimisho ya Sinodi ya Maalum
ya Maaskofu kuhusu Familia itakayofanyika mjini Vatican, mwezi Oktoba, 2014. Wanasema,
dhamana na utume wa Kanisa kwanza kabisa na kutangaza Habari Njema ya Wokovu kwa kuwapatia
watu fursa ya kukutana na Yesu, ili kuwakirimia utimilifu wa maisha. Ni Kristo anayeokoa
Familia kwa njia ya Kanisa lake.
Wajumbe na wahamasishaji wakati wa Semina
hii kwa pamoja wameangalia changamoto katika maisha ya ndoa na familia na kukiri kwamba,
umefika wakati kwa Mama Kanisa kuwaonjesha waamini na watu wote wenye mapenzi mema
ukuu na utakatifu wa maisha ya ndoa na familia, kwa kuwatangazia Injili ya Familia,
kwa kujikita katika ukweli unaofumbatwa ndani ya moyo wa mwanadamu.
Kardinali
Baldisserri amewashauri wajumbe wa Semina hii kutumia kipindi hiki cha maandalizi
ya Maadhimisho ya Sinodi Maalum ya Maaskofu kuhusu Familia, kuzungumzia kuhusu umuhimu
wa Familia katika maisha na utume wa Kanisa pamoja na kuwashirikisha wengine Mafundisho
ya Kanisa kuhusu Ndoa na Familia, yanayopaswa kutolewa ushuhuda katika uhalisia wa
maisha ya Wakristo. Sinodi ijayo, itajikita zaidi katika Mafundisho ya Kanisa kuhusu
Ndoa na Familia, kama njia ya kukukabiliana na changamoto zinazoendelea kujitokeza
kwa sasa. Familia za Kikristo zihamasishwe kuwapeleka watu kwa Kristo na Kanisa lake.
Mama
Kanisa anapojiandaa kwa ajili ya kumtangaza Mwenyeheri Yohane Paulo II kuwa Mtakatifu,
linatambua na kuthamini mchango mkubwa uliotolewa na Yohane Paulo II kwa ajili ya
kulinda, kutetea na kuendeleza Familia. Waraka wa Kitume, Wajibu wa Familia za Kikristo,
Familiaris Consortio, bado ni Waraka muhimu sana katika kukabiliana na changamoti
za maisha na utume wa Familia ndani ya Kanisa na Jamii katika ujumla wake. Waraka
huu ni Katekesi juu ya upendo wa kibinadamu, wanakiri wajumbe wa Semina hii.
Mwenyeheri
Yohane Paulo II ameutangazia ulimwengu ujumbe makini wa Ndoa na Familia inayopaswa
kusherehekewa katika mwanga wa neema ya Mungu, kwa kuendelea kutangaza Injili ya Familia
na uzuri wake, hata kama itapingana na mawazo ya watu wa nyakati hizi.
Kanisa
liwasindikize wanafamilia ili waweze kuwatangazia jirani zao ukweli na upendo wa maisha
ya ndoa na familia unaobubujika kutoka kwa Kristo na Kanisa lake. Mikakati ya shughuli
za kichungaji kwa ajili ya Familia ni sehemu ya maisha na utume wa Kanisa mahalia.
Hii ni changamoto kwa Wakristo kujitosa kimasomaso kutangaza Injili ya Furaha kama
ambavyo anaendelea kuhimiza Baba Mtakatifu Francisko kwa nyakati hizi.
Washiriki
wa semina hii, walikwenda kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican ili kutoa
heshima yao kwa Mwenyeheri Yohane Paulo II kwa njia ya Ibada ya Misa Takatifu iliyoongozwa
na Kardinali Carlo Caffarra, Rais wa kwanza wa Taasisi ya Ndoa na Familia ya Yohane
Paulo II, kuzunguka kaburi la Mwenyeheri Yohane Paulo II, lililoko ndani ya Kanisa
kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican.