2014-03-25 09:21:32

Wananchi wanaelemewa na umaskini, wanahitaji kuona ukuaji wa uchumi na maendeleo ya watu!


Kwaresima ni kipindi cha toba na wongofu wa ndani, ni muda muafaka wa kumtafuta Mungu ili kuweza kujipatanisha naye pamoja na jirani. Ni wakati wa kuimarisha ari na moyo wa kimissionari, ili kushuhudia uwepo wa Mungu kati ya watu wake. Myumbo wa uchumi kimataifa unaendelea kusababisha umaskini mkubwa wa hali na kipato, kiasi kwamba, kuna maelfu ya watu hawana uhakika wa kupata mahitaji yao msingi kutokana na ukosefu wa fursa za ajira.

Ni changamoto kwa Serikali ya Italia kuhakikisha kwamba, inajielekeza zaidi katika uzalishaji na upatikanaji wa fursa za ajira ili kuwajengea vijana matumaini ya leo na kesho iliyo bora, kwani kwa sasa wengi wao wamekata tamaa! Mkakati huu unawezekana ikiwa kama, Serikali itaendelea kubana matumizi kwa kuwekeza zaidi katika ukuaji wa uchumi na maendeleo ya watu.

Hayo yamesemwa na Kardinali Angelo Bagnasco, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Italia wakati wa kufungua mkutano mkuu wa Kamati kuu la Baraza la Maaskofu Italia, siku ya Jumatatu, tarehe 24 Machi 2014. Anasema, athari za myumbo wa uchumi kimataifa umepelekea pia mpasuko wa maisha katika familia nyingi nchini Italia na kwamba, hali ya umaskini wa hali na kipato inazidi kuongezeka kwa kasi kubwa nchini Italia. Huu ni umaskini unaojikita katika maisha ya kiroho na adili.

Baraza la Maaskofu Katoliki linalaani vitendo vya uvunjifu wa amani vinavyofanywa na baadhi ya wanasiasa wenye misimamo mikali, inayojikita katika ubinafsi, bila kuzingatia utu na heshima ya binadamu; usawa na haki. Kila mtu anayo haki ya kujieleza, lakini pia anapaswa kuwaheshimu wengine. Kuna haja kwa wanasiasa nchini Italia kusimama kidete kulinda na kutetea zawadi ya uhai tangu pale mtoto anapotungwa mimba tumboni mwa mama yake hadi mauti ya kawaida inapomfika kadiri ya mpango wa Mungu. Watu waondokane na ubinafsi usiokuwa na mashiko kwa kujenga na kuimarisha udugu, umoja na mshikamano.

Kardinali Bagnasco anasema kuna haja ya kuelimisha akili na moyo, kwa kukazia dhamiri nyofu na uhuru wa kuabudu. Wazazi na walezi wana haki ya kuchagua elimu wanayotaka kwa ajili ya watoto wao, ndiyo maana, hapo tarehe 10 Mei 2014, Baraza la Maaskofu Katoliki Italia, Wazazi, Walezi, wanafunzi pamoja na watu wenye mapenzi mema, wataungana na Baba Mtakatifu Francisko kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro kukazia umuhimu wa: maisha, familia na elimu makini kwa watoto. Kardinali Bagnasco anawaalika wazazi na walezi kusimama kidete kulinda na kutetea haki zao msingi.







All the contents on this site are copyrighted ©.