2014-03-25 11:41:22

Vitendo vya kigaidi nchini Kenya vinaendekezwa na umaskini miongoni mwa vijana!


Askofu Emmanuel Barbara wa Jimbo Katoliki Malindi na Msimamizi wa kitume Jimbo kuu la Mombasa, Kenya anasema, mashambulizi ya kigaidi yanayoendelea kujitokeza kwenye mwambao wa Pwani ya Mombasa yanatishia amani na usalama kwa wananchi wote wa Kenya na wala si tu kwa Wakristo.

Jumapili iliyopita, watu sita walifariki dunia na wengine ishirini na moja kujeruhiwa vibaya baada ya watu wanaosadikiwa kuwa ni kikundi cha Kigaidi kuvamia na kulipua Kanisa la Kiinjili huko Likoni. Inasadikiwa kwamba, vikundi hivi vya kigaidi vinafadhiliwa na baadhi ya wafanyabiashara wa Mombasa kwa ajili ya mafao yao binafsi.

Kuna vijana kutoka Somalia na Kenya wanaopewa fedha ili kufanya vurugu na wala si kwamba, ni waamini wenye msimamo mkali wa kidini kama wanavyotaka kuwasadikisha wananchi wengi wa Kenya. Askofu Barbara anasema, kuna haja kwa watu kutubu na kuongoka ili kuachana na vitendo vya kigaidi vinavyoendelea kusababisha maafa makubwa kwa watu na mali zao.







All the contents on this site are copyrighted ©.