2014-03-25 08:48:22

Simameni kidete kulinda na kutetea Injili ya Uhai!


Baraza la Maaskofu Katoliki Perù katika Maadhimisho ya Siku kuu ya Bikira Maria kupashwa habari na Malaika kwamba, atakuwa ni Mama wa Mungu, sanjari na Siku ya Injili ya Uhai Duniani, waamini pamoja na watu wenye mapenzi mema wanaalikwa kusimama kidete kulinda na kutetea Injili ya Uhai, inayokabiliana na utamaduni wa kifo unaokumbatiwa na sera za utoaji mimba na kifo laini. RealAudioMP3

Maaskofu kutoka Perù wanamwomba Bikira Maria awafundishe kupenda na kuthamini zawadi ya maisha, tangu pale mtoto anapotungwa mimba tumboni mwa mama yake. Familia zijifunze kuwapokea watoto na hatimaye kuwaonjesha upendo. Wanawake wawe na upendo mkamilifu kwa zawadi ya maisha wanayoibeba tumboni mwao, wakitambua na kuthamini dhamana na wajibu waliokabidhiwa na Mwenyezi Mungu wa kutunza zawadi ya uhai tumboni mwao.

Wanawake waguswe na upendo wa Kikristo na kamwe wasielemewe na: ubinafsi, utamaduni wa kifo pamoja na kumezwa na malimwengu kiasi cha kuonesha ukatili kwa watoto wao ambao bado hawajazaliwa. Watoto hawa wana haki zao msingi kama binadamu, kumbe, wasibaguliwe, wasidhalilishwe wala kubezwa na wale wanaowazunguka.

Baraza la Maaskofu Katoliki Perù linawaalika waamini, vyama vya kitume na watetezi wa haki msingi za binadamu kuunga mkono juhudi za Kanisa katika kulinda na kutetea Injili ya Uhai. Tarehe 25 Machi, Kanisa linapenda kuonesha umuhimu wa kulinda na kutetea Injili ya Uhai.

Hii ni fursa makini ya kutambua na kuthamini utu na heshima ya binadamu aliyeumbwa kwa sura na mfano wa Mungu na kwamba, maisha ni zawadi ya Mungu kwa binadamu. Maisha ya mtoto mchanga ambaye bado yuko tumboni mwa mama yake ni matakatifu, kamwe watu wasithubutu kuyachezea!








All the contents on this site are copyrighted ©.