2014-03-24 08:16:32

Siku ya Uhai Duniani na changamoto zake!


Kila siku Kanisa hukumbuka Fumbo la kuzaliwa Bwana linaposali Sala ya Malaika wa Bwana. Bikira Maria alikubali kuwa ni Mama wa Mungu, baada ya kusikia wito kutoka kwa Mwenyezi Mungu kwa njia ya Malaika Gabrieli. Tangu wakati huo Bikira Maria akawa ni Tabernakulo ya kwanza ya Neno wa Mungu aliyefanyika mwili. Hii ni Sherehe inayoadhimishwa na Mama Kanisa kila mwaka ifikapo tarehe 25 Machi. RealAudioMP3

Kwa mwaka huu Sherehe hii ina uzito wa pekee Mama Kanisa anapojiandaa kuadhimisha Sinodi maalum ya Maaskofu kwa ajili ya Familia, ili kuweza kukabiliana na changamoto za kichungaji zinazoendelea kujitokeza katika maisha na utume wa Familia sehemu mbali mbali za dunia.

Katika Maadhimisho ya Sherehe hii sanjari na Siku ya kuenzi Uhai, Baraza la Maaskofu Katoliki Hispania katika ujumbe wake kwa waamini na watu wenye mapenzi mema katika Siku ya Kuenzi Uhai, linawataka waamini kusimama kidete kuenzi Injili ya Uhai, chemchemi ya matumaini mapya katika kipindi cha myumbo wa uchumi kimataifa. Maaskofu wanaialika Familia ya Mungu nchini Hispania kukumbatia Injili ya Uhai na kuachana na utamaduni wa kifo, kwa ajili ya mafao na ustawi wa Hispania, Ulaya na dunia katika ujumla wake.

Hii ni dhamana inayowawajibisha kimaadili kupokea na kuikumbatia zawadi ya uhai kwani ni rasilimali kubwa katika kuleta mabadiliko katika sekta mbali mbali za maisha ya mwanadamu. Mataifa makubwa yaliyokuwa yameaathirika kutokana na maafa mbali mbali yaliweza kusimama tena kwa kutumia rasilimali watu, iliyokuwepo. Hii ndiyo nguvu kazi iliyoweza kuleta mabadiliko makubwa katika ukuaji wa uchumi na maendeleo ya mataifa haya.

Maaskofu wanasema, Hispania inakabiliwa na idadi ndogo sana ya watoto wanaozaliwa, hali inayotia wasi wasi kwa ajili ya ustai wa Jamii kwa siku za usoni. Kumbe kuna haja ya kuwa na mpango mkakati wa kiuchumi, kijamii na maisha ya kiroho kuwasaidia vijana wa kizazi kipya kutambua na kuenzi zawadi ya ndoa na maisha ya kifamilia. Serikali na wadau mbali mbali hawana budi kupanga sera na mikakati itakayoziwezesha Familia kutekeleza dhamana na wajibu wake barabara.

Maaskofu wanasema, jambo la msingi zaidi ni watu kubadili mtazamo na mtindo wa maisha kwa kujikita katika uhuru unaowajibisha kwa kuwahamasisha kujitoa kwa ajili ya maisha ya ndoa na familia katika upendo wa dhati. Hii nichangamoto kwa familia kuoneshana na kumegeana upendo kati yao na wale wote wanaowazunguka. Hivi ndivyo anavyoendelea kukazia Baba Mtakatifu Francisko kwa watu wa ndoa na familia.

Ikiwa kama Jamii itashindwa kuwasaidia watoto na wazee, haina mizizi ya matumaini kwa siku za usoni. Utu na heshima ya binadamu inapaswa kuheshimiwa, kuthaminiwa na kulindwa tangu pale mtoto anapotungwa mimba tumboni mwa mama yake hadi mauti ya kawaida yanapomfika kadiri ya mpango wa Mungu.

Baraza la Maaskofu Katoliki Hispania linawaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema kufanya tafakari ya kina kuhusu familia kama chemchemi ya matumaini mapya, changamoto na mwaliko wa kupokea kwa imani na matumaini zawadi ya maisha.

Waamini na watu wote wenye mapenzi mema, wanachangamotishwa na Mama Kanisa kusimama kidete kulinda na kutetea Injili ya Uhai, dhidi ya majanga ya kiuchumi na kijamii yanayoweza kujitokeza kwa kukumbatia utamaduni wa kifo. Watoto na vijana wa kizazi kipya wanazungukwa na mambo mengi ambayo yanawakatisha tamaa hata kuweza kufanya maamuzi magumu siku za usoni, lakini Baraza la Maaskofu Katoliki Hispania linawaalika kugundua zawadi ya uhai kama chemchemi ya matumaini mapya.

Imehaririwa na
Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.