2014-03-24 10:22:29

Rais Goodluck Jonathan wa Nigeria akutana na kuzungumza na Papa Francisko mjini Vatican


Baba Mtakatifu Francisko, Jumamosi tarehe 22 Machi 2014 amekutana na kuzungumza na Rais Goodluck Jonathan wa Nigeria. Viongozi hawa wawili katika mazungumzo yao wamelipongeza Kanisa kutokana na mchango wake wa hali na mali katika sekta ya elimu, afya na maendeleo endelevu ya wananchi wa Nigeria katika ujumla wao.

Wamekazia umuhimu wa kukuza na kuendeleza majadiliano ya kina kati ya makundi mbali mbali nchini Nigeria kwa ajili ya kudumisha haki, amani na upatanisho wakitaifa. Viongozi hao wamekazia kwa namna ya pekee kabisa umuhimu wa kusimama kidete kulinda na kudumisha utu, haki msingi za binadamu pamoja na uhuru wa kuabudu. Wamelaani vitendo vya mauaji ya watu wasiokuwa na hatia vinavyoendelea kushamiri nchini Nigeria kila kukicha!

Rais Jonathan na ujumbe wake walikutana pia na kuzungumza na Kardinali Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican aliyeambatana na Askofu mkuu Dominique Mamberti, Katibu mkuu wa mambo ya nchi za nje na ushirikiano wa kimataifa mjini Vatican.

Askofu mkuu Ignatius Ayau Kaigama, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Nigeria, amesema kwamba, kwa sasa wananchi wa Nigeria wamechoshwa kusikia mabadiliko ya mbinu mkakati wa kupambana na kikundi cha kigaidi cha Boko Haram, kwani kwa sasa wanataka kuona vitendo kwamba, magaidi wanashughulikiwa kikamilifu kisheria. Mkakati huu hauna budi kwenda sanjari na maboresho ya sera na vipaumbele katika masuala ya maendeleo ya watu kiuchumi na kijamii, ili kukidhi mahitaji msingi ya watu katika eneo la Kaskazini mwa Nigeria.

Nigeria kwa sasa imezindua mbinu mkakati mpya ambao umeandaliwa katika kipindi cha mwaka mmoja na nusu uliopita, kwa kushirikiana na “nguri” kutoka mataifa mbali mbali katika kupambana na kikundi cha kigaidi cha Boko Haram ambacho kwa sasa kimekuwa nitishio kubwa kwa watu na mali zao nchini Nigeria. Utekelezaji wa mkakati huu hauna budi kufanyika mapema iwezekanavyo kwani, mambo yanazidi kuwa magumu kila kukicha anasema Askofu mkuu Kaigama.

Wananchi wengi wa Nigeria wanataka kuona amani na utulivu, usawa na utawala wa sheria ukishika mkondo wake. Kanisa linaendelea kusali ili kweli amani na utulivu viweze kurudi tena nchini Nigeria.








All the contents on this site are copyrighted ©.